Tangazo

April 24, 2012

Auawa na Wananchi wenye Hasira kwa Tuhuma za Wizi wa Mifugo Mkoani Dodoma

RPC Dodoma, SACP Zelothe Steven
Luppy Kung’alo na Silyvester Onesmo wa Jeshi la Polisi Dodoma

Mtu  mmoja aliyefahamika kwa jina la RICHARD NGALYA mwenye umri wa miaka 33,   Mkazi wa Mpunguzi katika Manispaa ya Dodoma,   Mkulima anayetuhumiwa kuwa mwizi maarufu wa Mifugo ameuawa  na wananchi wenye hasira kali baada ya kukutwa akitaka kuiba Ng’ombe katika Zizi.

Akizungumzia tukio hilo  Kamanda wa Polisi  Mkoa wa Dododma, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Bw. Zelothe Steven alisema  tukio hilo lilitokea siku ya Jumatatu majira ya saa nane usiku  ambapo mwizi huyo  alikutwa katika Zizi la Ng’ombe mali  ya Bw.  YOHANA MAN’GONDA miaka (89) akilifungua  kwa lengo la kuiba ng’ombe.

Kamanda Zelothe Steven alisema marehemu alikutwa na watoto  wawili wa Mzee mwenye zizi hilo, ambaye aliwaagiza watoto wake  kulilinda baada ya siku moja kabla ya tukio la kuuwawa, marehemu alikutwa na vijana hao katika jitihada za kutaka kulifungua zizi hilo.

Hivyo  siku ya tukio watoto hao, wakiwa katika ulinzi, ndipo walipomkuta mwizi huyo wa mifugo na kupiga yowe, ambapo majirani na watu wengine wakaribu wakatoka na kumfukuza hadi katika mlango wa nyumbani na mwizi huyo ambapo walimshushia kipigo kikali.

“Baada ya Kumpa kipigo hicho walimkamata na kumpeleka  kwa viongozi wa kijiji hicho cha Mpunguzi, ambapo alipofikishwa katika ofisi za kijiji alifariki dunia” aliongeza Kamanda Zelothe Steven.
 
Hata hivyo Kamanda huyo wa Polisi Mkoa wa Dodoma, alikemea vikali hatua na  vitendo vya wananchi kujichukulia sheria mikononi , na kusema kuwa  kinyume kabisa na haki za msingi  za binadamu pamoja na sheria za nchi kwa ujumla.

Aidha aliwataka wananchi kutekeleza dhana nzima ya utii wa sheria  bila shuruti, inayotaka mwananchi kutekeleza sheria pasipo matumizi ya nguvu zinazoweza kuleta madhara kwa binadamu kutumika.

Aliwataka  wananchi hao kuacha kujichukulia sheria mikononi na kutoa wito kwao wa kutoa taarifa katika vituo vya Polisi vilivyo jirani mara  matukio ya uhalifu yanapotokea katika maeneo yao ili hatua za msingi  za kutekeleza sheria zifuatwe.

Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana kwa wanakijiji hicho, walidai mwizi huyo alikuwa mzoefu na kwamba alishawahi kufungwa kwa kosa la wizi wa mifugo, ambapo alihukumiwa miaka thelathini (30) jela ambapo alitumikia miaka nane na kutoka  kwa rufaa mwaka jana.

No comments: