Tangazo

November 29, 2012

SERIKALI YAZINDUA BARAZA LA WATAALAM WA KUREKEBISHA UPEO WA MACHO KUONA

Dk. Hussein Mwinyi
- Pia yakabidhi Magari tisa na Pikipiki 107 kusaidia huduma za Afya

 Na Aron Msigwa –MAELEZO

Dar es salaam.

Serikali imezindua rasmi baraza la wataalam wa kurekebisha upeo wa macho kuona nchini kwa lengo la kusimamia, kudhibiti na kuratibu utoaji wa huduma bora za macho nchini litakalofanya kazi zake kwa mujibu wa sheria ya Optometria Na.12 ya mwaka 2007.

Akizindua baraza hilo lenye wajumbe 12 leo jijini Dar es salaam, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dkt. Hussein Mwinyi amesema kuwa baraza hilo lina wajibu wa kuhakikisha kuwa huduma bora za macho zinaendelea kutolewa kwa kuzingatia taratibu na viwango vilivyowekwa pia kuzingatia umuhimu wa macho katika mwili wa binadamu.

Amesema maisha ya kila siku ya binadamu yanategemea uono wa macho na kuongeza kuwa hali ya kutoona inasababisha maisha ya mwanadamu kuwa hatarini na wakati mwingine kupoteza nguvu kazi ya taifa na kurudisha nyuma maendeleo ya taifa.

"Kila mmoja wetu anafahamu umuhimu wa macho kikiwa kiungo muhimu sana katika mwili wa binadamu kama vilivyo viungo vingine na tusipoona kutokana na matatizo ya macho maisha yetu yanakuwa hatarini".

Amefafanua kuwa baraza hilo lina wajibu wa kuhakikisha kuwa watoa huduma na wapokea huduma wanakua na uhusiano mzuri na kulitaka baraza hilo kutoa elimu ya afya ya macho kwa wananchi juu ya namna ya kutunza macho yao kabla ya madhara kutokea.

Dkt. Mwinyi amesema licha ya Tanzania kukabiliwa na changamoto ya uhaba wa wataalam wa macho serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha kuwa huduma za macho zinawafikia wananchi wengi hasa maeneo ya vijijini.

Amelitaka baraza hilo kuweka mikakati ya kukabiliana na biashara holela ya miwani isiyokidhi viwango iliyoenea hapa nchini kwa kushirikiana na Halmashauri za manispaa ili kuondoa hatari inayoweza kulikumba taifa kutokana na kutumia miwani isiyokidhi viwango.

"Hivi sasa biashara ya miwani inayouzwa na wamachinga imeenea kila mahali nchini, jambo hili ni hatari kwa afya ya macho kwa watanzania nafahamu linatokana na utandawazi uliokithiri lakini ninyi kama baraza lazima mtafute mbinu ya kukabiliana nalo" amesisitiza.

Kwa upande wake mwenyekiti wa baraza hilo Bw. Adam Simbeye amesema kuwa baraza hilo jipya linachukua nafasi ya baraza lililozinduliwa mwaka 2009 na kudumu kwa muda wa miaka 3.

Amesema pamoja na mambo mengine baraza hilo katika kipindi cha miaka 3 limefanikiwa kujenga na kulinda maadili ya watumishi wa fani hiyo, kulinda na kudhibiti vituo vya kutolea huduna, kufanikisha zoezi la kusajili vituo vya kutolea huduma nchini na kuhamasisha utii na ufuataji wa kanuni na taratibu za taaluma.

Aidha amesema kuwa baraza linakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa fedha na kukosa ofisi maalum ya kuendesha majukumu yake, aidha amesema baraza hilo limeshindwa kusimamia suala la wafanyabisahara ndogo ndogo (wamachinga) kuuza miwani holela mitaani.

Kwa upande wake mjumbe wa baraza hilo Bw. Anamringi Macha akizungumza kwa niaba ya wajumbe wenzake amesema kuwa uzinduzi wa baraza hilo unawapa nguvu kisheria kutekeleza majukumu yake kwa kipindi cha miaka 3.

Amesema watafanya kazi kwa uadilifu kwa lengo la kuhakikisha kuwa watanzania wote wanapata huduma bora za macho kwa mujibu wa kanuni tarattibu na viwango vilivyowekwa.

"Kuzinduliwa kwa baraza hili kunatupa nguvu kisheria kusimamia, kudhibiti na kuhakikisha huduma za macho nchini zinatolewa kwa viwango na kwa kuzingatia kanuni na taratibu na hili ndilo jukumu letu kuhakikisha maisha na afya za watanzania zinakua salama" Amesema.

Wakati huo huo serikali kwa kushirikiana na shirika la UNFPA, Mfuko wa Dunia na serikali ya Uholanzi imekabidhi magari 9 ya kubebea wagonjwa na pikipiki 107 kwa ajili ya kurahisisha huduma za ukusanyaji wa taarifa za afya, kusafirisha wagonjwa na kuboresha huduma za afya ya mama na mtoto katika maeneo mbalimbali nchini.

Akikabidhi magari hayo kwa wawakilishi wa hospitali zilizopewa magari na pikipiki hizo Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dkt. Hussein Mwinyi amesema magari na pikipiki hizo yamegharimu fedha nyingi na kuwataka viongozi ambao maeneo yao yamepewa vifaa hivyo kuvitunza ili vidumu na kuendelea kutoa huduma husika.

" Vifaa vilivyo katika magari haya vinatakiwa kutunzwa ili visiharibike au kuibwa ni muhimu sana kukabidhiana kwa maandishi kila inapotokea watumishi wanabadilishana zamu za kutoa huduma katika magari haya" amesisitiza Dkt. Mwinyi.

Amesema magari yenye vifaa vyote yamegharimu shilingi milioni 250 kila moja na yatapelekwa kutoa huduma ya kubebea wagonjwa katika Taassisi ya Mifupa nchini (MOI), Hospitali ya KCMC ,Hospitali za wilaya ya Maswa, Hospitali ya mama Maria wa Kanisa na wilayani Longido.

Aidha amesema magari mengine yatapelekwa katika vituo vya afya wilayani Kahama na Bukombe na kuongeza kuwa baadhi ya pikipiki zilizonunuliwa tayari zimepelekwa katika halmashauri 26 nchini.

Pia amesema kuwa katika kuhakikisha kuwa wagonjwa wanaobebwa katika magari hayo wanakuwa salama hata kama hali zao ni mbaya wizara kwa kutumia wataalam wake imeandaa orodha ya vifaa vinavyotakiwa kuwemo katika gari linalotumiwa kubeba wagonjwa na kusambaza orodha ya vifaa hivyo kwa wadau husiDk. Hussein Mwinyi

No comments: