Tangazo

July 24, 2017

Dk. Kigwangalla: Serikali itaendelea kuboresha makazi ya Wazee nchini

Dk. Kigwangalla: Serikali itaendelea kuboresha makazi ya Wazee nchini, aweka jiwe la msingi la ujenzi makazi ya Wazee Kolandoto Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla amesema Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi (CCM), itaendelea kusimamia haki za wananchi wake kuanzia watoto, Vijana na Wazee ilikulinda haki na hutu wao hapa nchini. 

  Dk. Kigwangalla amesema hayo Julai 22,2017, wakati alipokuwa mgeni rasmi katika shughuli ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa bweni la makazi ya Wazee ya Kolandoto, yaliyopo umbali wa zaidi ya KM 10, kutoka Shinyanga Mjini, mkoani Shinyanga. 

  Ambapo mbali na kuweka jiwe hilo la msingi la ujenzi wa bweni hilo, pia alifungua rasmi jiko maalum la gesi ambalo litakuwa likitumika kwa ajili ya chakula cha wazee hao pamoja na kukabidhi Bajaji ya miguu mitatu itakayorahisisha usafiri kwa wazee hao kwenye makazi yao hayo. Makazi ya wazee ya Kolandoto ni ya muda mrefu, ambapo kwa uanzishwaji wa ujenzi wa bweni hilo litakuwa faraja kwa wazee wanaoishi hapo kwani litakuwa na uwezo wa kuchukua wazee zaidi ya 20.

“Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania imeweka msisitizo kuendelea kuwaenzi wazee kwa michango yao katika kulijenga taifa letu. Serikali ina jukumu la kuwatambua wazee na kuwapatia huduma za matibabu bila malipo na kuhakikisha wanalindwa dhidi ya vitendo vya ukatili ikiwemo mauaji. Katika kutekeleza haya, Serikali ya Awamu ya tano imeunda Wizara inayosimamia masuala ya wazee ili kuhakikisha haki zao zinalindwa. Katika kufanikisha azma hiyo, serikali inahudumia makazi hayo 17 ya wazee wasiojiweza hapa nchini” alieleza Dk. Kigwangalla 

  Mpaka likikamilika litatosha kuwahudumia wazee wasiojiweza 20. Hivi sasa kuna wazee 16, kituoni hapa. Majengo ya zamani ni ya udongo na yamekaa zaidi ya miaka 50 bila ukarabati. Kimsingi hayafai tena kwa matumizi ya binadamu (yapo condemned). Tumeyakarabati ili yaweze kutumika wakati tukijenga jengo hili jipya la kisasa” alieleza Dk. Kigwangalla.

Dk. Kigwangalla aliongeza kuwa, Pamoja na ujenzi wa jengo hilo kwenye makazi ya wazee wasiojiweza, Wizara yake imefanya maboresho makubwa na muhimu sana kwenye makazi hayo ikiwemo kuweka majiko ya kisasa ya gesi, vyombo vya kupikia na kulia chakula, huduma ya maji, vifaa vya huduma ya kwanza, vifaa vya chumba cha kulala na vyombo vya usafiri (Bajaj)na huduma muhimu kwa wazee hao. 

  Hata hivyo, Dk. Kigwangalla ameeleza pamoja na ufinyu wa bajeti wanayopewa kwa ajili ya idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii, amewapongeza wataalamu wa idara hiyo wakiongozwa na Katibu Mkuu, Ndg. Sihaba Nkinga, kwa ubunifu uliowezesha kufanyika bila kupokea pesa ya kutekeleza miradi ya maendeleo. 

  “Wataalamu wanapaswa kutumia ujuzi wao kuleta tija na ufanisi kwenye utekelezaji wa majukumu tuliyopewa. Nawapongeza sana kwa kufanya jambo hili kubwa na la umuhimu” alimalizia Dk. Kigwnagalla. 

  Hata hivyo, Dk. Kigwangalla amesema kuwa, Serikali itaendelea kuimalisha makazi ya wazee hao kwani inatambua thamani yao hivyo ni jukumu la kuwasaidia huku pia akitoa rai kwa Jamii kuweza kukaa nao wazee hao kwani Uzee unapitiwa na jamii yote na haukwepi. 

  Kwa Mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012, Tanzania inakadiriwa kuwa na Wazee 2,507,568 (Wanawake 1,307,358, Wanaume 1,200,210) sawa na asilimia 5.6 ya wananchi wote. 

Aidha, kwa mujibu wa Sensa hiyo idadi hiyo inakadiriwa kuongezeka hadi kufikia wazee 2,777,002 (wanawake 1,447,659, wanaume 1,329,343) ifikapo Disemba, 2017. Ongezeko hili la idadi ya wazee ni kiashiria cha kuendelea kuimarika kwa hali ya upatikanaji wa huduma za msingi kwa jamii ikiwemo huduma ya afya upatikanaji wa chakula na huduma bora za matibabu; hivyo kuchangia kuongezeka kwa umri wa kuishi. 

  Hadi sasa Serikali Serikali inahudumia makazi 17 ya wazee wasiojiweza na ambao hawana ndugu na jamaa ikiwemo kituo hicho cha Kolandoto, Mkoani Shinyanga.
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla akifungua rasmi jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa Bweni la Wazee wasiojiweza la Kolandoto, Mkoani Shinyanga mapema jana Julai 22,2017
Bweni hilo la Wazee wasiojiweza linaloendelea kujengwa katika makazi ya Kolandoto, Mkoani Shinyanga
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla akipatiwa maelezo ya ujenzi wa bweni la Wazee Kolandoto
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla akikagua makazi ya wazee Kolandoto
Baadhi ya Wazee na watu mbalimbali waliojitokeza katika tukio hilo
Mwenyekiti wa Wazee wa makazi ya Wazee Kolandoto akitoa salamu za pongezi kwa niaba ya Wazee wanaolelewa kituoni hapo
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla akimpongeza Mwenyekiti wa Wazee wa waaolelewa kituo cha Kolandoto
Mhe. Nyabaganga Talaba – Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga akizungumza katika mkutano huo
Baadhi ya majengo ya zamani ya kituo cha Wazee wasiojiweza cha Kolandoto yanavyoonekana
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla akioneshwa chumba maalum cha mitungi ya gesi kilichojengwa kwa ajili ya kusaidia makazi ya wazee Kolandoto
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla akifungua rasmi jiko maalum la gesi kwa ajili ya kupikia vyakula vya Wazee wasiojiweza wa Kolandoto
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla akikata utepe wakati wa kukabidhi Bajaji kwa kambi hiyo ya Wazee Kolandoto
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla akikata utepe kwa ajili ya kukabidhi madawa na kisanduku cha huduma ya kwanza
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla akihutubia katika mkutano huo
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla akimpongeza mmoja wa Wazee wanaopatiwa huduma katika makazi hayo ya Kolandoto
Katibu Mkuu Maendeleo ya Jamii,Bi. Sihaba Nkinga akizungumza katika tukio hilo
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Mh. Dk.Hamisi Kigwangalla akifurahia jambo na baadhi ya Wazee wanaopatiwa huduma katika makazi hayo ya Kolandoto wakati wa tukio la kuweka jiwe la msingi la bweni litakokuwa na uwezo wa kuchukua Wazee zaidi ya 20.

No comments: