Tangazo

February 28, 2018

MJADALA WA KITAIFA UNAHITAJIKA KUHUSU FAIDA ZA MATUMIZI YA MBEGU ZA GMO KATIKA KILIMO

 Mwenyekiti wa Kavazi la kwanza la Mwalimu Nyerere kwa mwaka 2018 Dkt. Ng’wanza Kamata ambaye ni mahadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDSM), akichokoza mada kuhusu matumizi ya mbegu za GMO na teknolojia ya uhandisi jeni katika kilimo. Kulia ni Dk.Richard Mbunda  kutoka UDSM. 
 Wadau wakiwa kwenye mkutano huo uliofanyika Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia ((COSTECH) Dar es Salaam jana.
 Mkutano ukiendelea.
 Dk.Richard Mbunda  kutoka UDSM, akielezea changamoto mbalimbali zitokanazo na matumizi ya mbegu za GMO katika kilimo.

Usikivu katika mkutano huo. 
 Dkt. Aloyce Kulaya akichangia jambo kwenye mkutano huo.
 Dkt. Adolphine Kateka akichangia.
 Dkt. Goodluck Ole Medeye, akielezea umuhimu wa mbegu hizo katika kilimo.
 Alfred Mmbaga kutoka Tanzania Meat Board akichangia mada.
  Elisa  Greebe kutoka Chuo Kikuu cha Leeds akichangia.
 Mkulima mdogo Ernest Likoko akichangia mada.
 Dk Emmarold Mneney akichangia mada kwenye mkutano huo.
 Emma Nyerere kutoka Taasisi ya Pawo Pan African Women Organisation Tanzania akichangia jambo.
 Dkt. Nicholous Nyange, akizungumza kwenye mkutano huo.
Mada zikichangiwa.
Dkt.Roshan Abdallah kutoka Agricultural Innovation Research Foundation Tanzania, akichangia jambo.

Na Mwandishi Wetu

WASHIRIKI wa Kavazi la kwanza la Mwalimu Nyerere kwa mwaka 2018 wameomba elimu zaidi itolewe kwa jamii ili kusaidia kuwa na uelewa wa pamoja kama nchi katika kuelekea kutumia teknolojia ya uhandisi jeni kukablina na changamoto zinazomkabili mkulima nchini kwa sasa na kuinua tija.

Wakichangia mjadala huo uliolenga kuangalia nafasi ya mbegu za GMO na teknolojia ya uhandisi jeni katika kilimo wadau hao kutoka sekta na taasisi mbalimbali nchini wamesema pamoja na jitihada kubwa zinazofanywa na watafiti kwa kushirikiana na serikali na makampuni mengine ya nje jamii inahitaji kuelimishwa ili kuondokana na mashaka ambayo yamekuwa yakizunguzwa na baadhi ya wadau kuhusu mbegu hizo.

Wamesema wakulima wengi uzalishaji wao ni mdogo kutokana na  kutumia zana duni,kutozingatia kanuni bora za kilimo,Mbegu zisiszo bora  na teknolojia zingine ambazo zimewafanya wakulima kuendelea kubaki palepale na kuona kilimo sio kazi yenye tija na thamani kama kazi zingine na hivyo wadau hao kuomba mjadala mpana ufanyike wa kitaifa kuhusu teknolojia ya GMO na kuona kama ina mchango katika kusaidia kumkomboa mkulima kutoka katika hali yake ya sasa.

Akizungumzia umuhimu wa mbegu hizo za GMO kwa taifa na wakulima nchini aliyekuwa (Waziri wa Mifugo na Uvuvi katika serikali ya awamu ya nne) ????? Dkt. Goodluck Ole Medeye alisema kuwa mchakato wa kuanza au kutokuanza kutumia mbegu za GMO ulianza zamani lakini serikali kupitia waalamu wake walikaa chini na kutathimini uhitaji wa teknolojia hiyo na kuona kuwa ni mkubwa na hivyo kuamua kuwapa nafasi watafiti kufanya kwanza utafiti ili kujiridhisha juu ya faida na hasara zake.

Alisema kuwa yeye binafsi alikuwa mtu wa kwanza kupinga matumizi ya mbegu zinazotokana na teknolojia hiyo lakini baada ya kuwapa nafasi watafiti kueleza na kuwaelimisha mawaziri na viongozi wengine wa serikali aliona kuwa hakuwa sahihi na kwa pamoja wakafikia uamuzi wa kuwaruhusu watafiti wafanye utafiti nchini ili kujiridhisha kuwa na uwezo wa kutambua mbegu na bidhaa zitokanazo na teknolojia hiyo.

Dkt. Medeye aliongeza kuwa hakuna namna ambayo Tanzania itakwepa kutumia mbegu hizo au bidhaa za GMO kwakuwa Tanzania sio kisiwa kama nchi zinazoizunguka Tanzania zinafanya tafiti kwa kasi na kutumia mbegu hizo basi Tanzania itajikuta wananchi wake wanatumia mbegu hizo kwani kwa sasa nguo nyingi tunazovaa zinatoka nchi zinazozalisha pamba ya GMO na baadhi ya vyakula  tunavyokula kutoka nje vinatokana na mbegu za GMO.

Waziri huyo wa zamani amebainisha kuwa wakulima wengi wa Tanzania kwa miaka nenda rudi bado wanazalisha chakula kidogo sana ambacho hakikidhi mahitaji ya kaya zao na kupata ziada kwaajili ya kuuza kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo zana dunia,kutotumia mbinu bora za kilimo na hasa mbegu bora hivyo ni wakati sasa nchi ikaona umuhimu wa kumuinua mkulima kwa kumpatia mbegu zenye kumletea matumani na tija.

Kwa upande wake mtafiti mstaaafu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia ((COSTECH) Dkt. Nicholous Nyange ambaye alikuwa mtafiti kwenye masuala ya tafiti za bioteknolojia za kilimo nchini aliyewasiliasha mada juu umuhimu wa teknolojia na mbegu za GMO amesema kuwa inakadiriwa kuwa Tanzania kwa sasa inawatu wapatao milioni 58 na idadi hii inaongezeka kila siku na kama sayansi haitatumika kusaidia kuzalisha chakula cha kutosha basi huenda taifa likasumbuliwa na njaa kila mwaka kwenye maeneo mengi.

Alisema wakulima pamoja na jitihada kubwa zinaofanywa na wakulima kulima na kupanua mashamba kila siku lakini bado hawajaweza kuzalisha chakula cha kutosha kutokana nasababu mbalimbali ikiwemo wadudu,magonjwa na changamoto zingine zinazotokana na mabadiliko ya tabia nchi ikiwemo Ukame kwenye maeneo mengi ya nchi kwa sasa.

Dkt,Nyange  amesema kawimu zinaonyesha kuwa Tanzania kwenye uzalishaji wa mahindi unakadiriwa kufikia ati ya tani 1.5 hadi tani mbili pale ambapo hali ya hewa na mtawanyiko wa mvua utakuwa mzuri lakini kwa nchi zilizoendelea kama vile marekani wanazalisha tani 8 hadi 9 kwa ekari kutokana na kutumia teknolojia za kisasa ili kuongeza uzalishaji .

Alisema kuwa pamoja na uchumi wa taifa kukua kwa silimia 7 lakini kilimo ambacho ndio uti wa mgongo wa mtanzania ambao zaidi ya asilimia 80 ya watanzania wanakitegemea chenyewe kinakua kwa asilimia 3 tu na hivyo kusema kuwa kama teknolojia ikitumika na wakulima wakawezeshwa kilimo kitaweza kuchangia vyema kwenye pato la taifa na kuwanufaisha wakulima ambao tunaona TASAF inawapa fedha kupitia mpango wa serikali wa kusaidia  kaya masikini.

Aliongeza kuwa eneo linalofaa kwa kilimo na makazi likigawanywa kwa idadi ya watu waliopo nchini katika kipindi kifupi kichacho halitatosha kupata maeneo ya kutosha kwaajili ya kilimo makazi na shughuli zingine za kibinadamu hivyo njia pekee ni kuwawezesha wanananchi na wakulima kutumia mbinu za kisasa kuzalisha kwa wingi kwenye maeneo madogo ili kuendana na ongezeko la idadi ya watu na eneo la nchi lililopo ambalo haliongezeki.

Kwa upande wake Dkt. Aloyce Kulaya mtafiti wa zao la mahindi mstaafu na mshauri wa mradi wa Water efficient Maize for Africa (WEMA) alisema kuwa suala la GMO linaangalia tuu kwenye vyakula lakini teknolojia hiyo inatumika zaidi kwenye kutengeneza madawa kama yale ya kisukari na kubainisha kuwa hata kama dawa ya ukimwi ikipatikana basi inaweza kuwa kwa kutumia njia hii pekee na sio nyingine.

Alisema teknolojia ya uhandisi jeni sio ndio njia pekee ya kupata ufumbuzi wa matatizo ya wakulima lakini pale mbinu za kawaida zinaposhindwa ndio teknolojia hiyo pekee hutumika katika kupata ufumbuzi wa haraka na sahihi wa changamoto za magonjwa,ukame na wadudu ambazo zinawasumbua wakulima nchi nzima ambayo binu za kawaida zimeshindwa.

Dkt. Kulaya aliongeza kuwa kwa wasiwasi wa watu kuwa mbegu za asili zitapotea hauna maana kwakuwa mbinu hizo za kuupatia mmea kinga na uwezo wa kuwa na sifa fulani kunaweza kufanyika pia kwenye mbegu zetu za asili na hivyo kuziwezesha mbegu hizo kuhimili magonjwa,wadudu na changamoto zingine na kumuwezesha mkulima kupata mazao ya kutosha.

Kwa upande wake Profesa, Rwaitama ameitaka serikali kuwezesha vituo vyetu vya utaifa nchini kuwa na uwezo wa kufanya tafiti hizi ambazo zinaweza kusaidia kuwainua wakulima kupambana na changamoto zinazowakabili badala ya kutegemea wafadhili pekee ambao wanapoleta fedha kwenye utafiti Fulani wanakuwa na vigezo vyao na sio lazima view kipaumbele cha nchi.

Alisema vituo vingi vya utafiti vya zamani vilikuwa vinafanya kazi nzuri katika kazi za utafiti lakini kwa sasa vimeshuka utendaji wake na kuonekana kuwa na mchango mdogo sana kwa maendeleo ya nchi ili kuweza kuwa na udhibiti wa kile kinachozalishwa kuwa mali ya taifa kwakuwa kitakuwa kimezalishwa kwa kutumia fedha za wananchi.

Prof. Rwaitama akitolea mfano wa utafiti wa Panya uliofanywa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) alisema ni moja ya matunda makubwa ambayo yanaipatia Tanzania na watafiti wake heshima kubwa katika kutumia panya kufanya kazi mbalimbali kubwa duniani kama vile kutambua mabomu,makohozi ya TB kwa haraka.

Naye Mwenyekiti wa mkutano huo Dkt. Ng’wanza Kamata ambaye ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDSM) alisema kuwa Kavazi la Mwalimu Nyerere litaendelea kufanya mijadala juu ya jambo hili kila mara ili kusaidia kuwepo kwa mjadala mpana katika kujadili faida na hasara za teknolojia ya Uhandisi jeni kabla teknolojia hiyo haijamfikia mkulima.

Alisema wananchi wote wakielewa vizuri jambo hili litasaidia kuondoa mashaka juu ya usalama wa teknolojia ambao umekuwa ukitolewa na watu mbalimbali na mashaka hayo yakiondoka ndipo sasa kila mtu anaweza kuwa huru kuchagua kuitumia teknolojia hiyo au la kwa manufaa yake na manufaa ya taifa kwa ujumla.

Profesa, Kamata aliongeza kuwa mashaka ni lazima kwa jambo lolote au teknolojia yoyote mpya inapoingia sokoni na huu ndio wakati muafaka wa watafiti kusikia mashaka na watu na kisha kuyatafutia majibu ya kisayansi kwani hakuna mtu anayeweza kufurahia jambo bila kuwa na wasiswasi hususani kwa teknolojia mpya yoyote.

Awali akiwasilisha mada yake ambayo ilitakiwa kujibiwa na Dkt. Nyange dhidi ya GMO mtafiti kutoka Chuo Kikuu cha Dar es salaamu, Richard Mbunda alisema bado kuna taarifa ambazo zinapishana katika kiwango ambacho mbegu za GMO zinazostahimili ukame ambazo zinefanyiwa majaribio kwenye kituo cha utafiti wa kilimo makutupora katika uwezo wake wa kupunguza hasara kwa mkulima.

Mbunda amesema mashaka makubwa wanayoyaona baadhi ya watu ni kuhusu usalama wa vyakula vinavyotokana na mbegu za GMO kama chakula kwa maana ya afya na mazingira mambo ambayo ni lazima watafiti wayaangalie na kujiridhisha kabla ya kuzipeleka mbegu hizo kwenye mamlaka za serikali zinazopitisha mbegu zote nchini.

Mtoa mada huyo alieleza wasiswasi wake na kutaka kujua juu ya namna mkulima mdogo atakavyoweza kunufaika na teknolojia hiyo ili isijemfanya mkulima kuwa mtegemezi wa mbegu kutoka nje ya nchi na kutaka kujua namna wakulima watakavyoweza kupata mbegu hizo kwa urahisi na bei nafuu pale ambapo zitapitishwa na kuwa mbegu ili kutumika hapa nchini.

MANAIBU WAZIRI MAVUNDE NA BITEKO WAFANYA ZIARA YA KUSHTUKIZA MGODI WA ALMASI MJINI SHINYANGA

Manaibu Waziri, Mhe. Antony Mavunde kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana na Ajira, (wapili kushoto), na  Mhe.  Dotto Biteko, kutoka Wizara ya Madini, (wapili kulia), wakipatiwa maelezo na Mjiolojia Mkuu wa mgodi wa Al-Hilal Minerals Limited wa mjini Shinyanga, (aliyenyoosha mkono), wakati wa ziara ya kushtukiza ya viongozi hao ili kubaini kama mgodi huo unazingatia sheria katika kutekeelza majukumu yake, Ziara hiyo waliifanya Februari 27, 2018

NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID, SHINYANGA

NAIBU Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, anayeshughulikia Kazi, Ajira na Vijana, Mhe. Antony Mavunde, na mwenzake wa Madini Mhe. Dotto Biteko, leo Februari 27, 2018 wamefanya ziara ya kushtukiza kwenye mgodi wa almasi wa Al-Hilal Mineral Ltd ulioko kilomita 60 kutoka mjini Shinyanga, ili kubaini kama wamiliki wa mgodi huo wanatekeleza sheria za uendeshaji.
Wakati Mheshimiwa Mavunde alikuwa akifuatilia kama mgodi huo umejisajili na Mfuko wa Fidia Kwa Wafanyakazi (WCF), ikiwa ni pamoja na jinsi mgodi huo unavyotekeleza Sheria ya ajira na mahusiano kazini,
Mhe. Biteko yeye alikuwa akifuatilia kwa nini mgodi huo haujawasilisha wizarani mpango wa ukarabati wa mazingira (rehabilitation plan) na mpango wa uwajibikaji wa shirika kwa jamii (Corporate Social Responsibility-CSR).
Kwa upande wake Mhe. Mavunde alibaini kuwa Mgodi huo bado ulikuwa haujajisajili na Mfuko na badala yake uongozi ulipeleka michango siku moja kabla ya ziara ya Naibu waziri.
“Serikali inataka waajiri wazingatie sheria, na ninyi mmevunja sheria kwa kutojisajili, ingawa mmelipa michango yenu jana, ninachoweza kusema, agizo la serikali la kuwafikisha mahakamani waajiri ambao hawajajisajili nchi nzima liko pale pale, ni juu yenu kutekeleza hilo kabla hamjapelekwa mahakamani.” Alisema Mhe. Mavunde.
Ziara ya Naibu Waziri ni muendelezo wa ziara yake iliyoanza Februari 26, 2018 jijini Mwanza ambapo aliagiza kufikishwa mahakamani waajiri watatu jijini Mwnaza.
Mhe. Mavunde ameagiza waajiri hao kufanya mawasiliano na watendaji wa Mfuko haraka iwezekanavyo ili kuweza kubaini kiwango cha riba kila mwajiri anachopaswa kulipa kutokana na kuchelewesha michango katika Mfuko. “Ni kosa la jinai kwa mwajiri kutotekelza takwa hilo la kisheria na kifungu cha 71(4) cha Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi kimeweka wazi kuwa mwajiri wa aina hii, anaweza kutozwa faini isiyozidi shilingi milioni 50,000, kifungo kisichozidi miaka 5 jela au adhabu zote kwa pamoja, kwa hivyo nitoe wito kwa waajiri hao, hakuna sababu ya kushurutishwa kutekeleza sheria.­­

Naibu Waziri Mvunde, akiwasikiliza wafanyakazi wa mgodi wa almasi wa Al-Hilal Minerals Limited wa mjini Shinyanga.
Mhe.Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, anayeshughulikia Kazi, Vijana na Ajira, Mhe. Antony Mavunde, (kushoto), akiwa na mwenzake wa Madini Mhe. Dotto Biteko, wakati akizungumza kwenye kikao cha pamoja baina ya uongozi wa mgodi huo kwenye ziara hiyo ya kushtukiza Februari 27, 2018
 Mhe. Biteko, (kulia), akiwa na Mhe. Mavunde, wakati akizungumza katika kkikao cha pamoja na uongozi wa mgodi huo.
Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, (WCF), Bw.Anselm Peter, (kushoto) na Naibu Kamish Idara ya Kazi, Bi.Rehema Moyo.
 Kutoka kushoto, Bw. Anslem Peter, Bi. Rehema Moyo, na Bi. Laura Kunenge 

 Mhe. Naibu Waziri akizungumza na baadhi ya wafanyakazi wa mgodi huo.

Mwanasheria wa WCF, Bw. Deo, (kushoto), Afisa Kazi Mfawidhi wa Mkoa wa Shinyanga, na Bw. Anslem peter
 Naibu Waziri Mvunde akizungumza na baadhi ya manesi wa hospitali ya Kolandoto.
 Naibu Waziri, akiongozana na Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Kolandoto, Dkt. Maganga Ngoi (katikati) na Mkurugenzi wa Uendeshaji WCF, Bw. Anslem Peter, wakati akitoka hospitalini hapo baada ya ukaguzi.
 Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Mhe.Josephine Matiro, (wapili kushoto), Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano WCF, Bi. Laura Kunenge, (wakwanza kushoto), na Afisa Kazi Mkoa wa Shinyanga, wakimsikiliza Bw. Anslem Peter.

Kaimu Kamishna kutoka Idara ya Kazi, Bi. Rehema Moyo, akifafanua masuala yahusuyo  Sheria ya ajira na mahusiano kazini, Kulia ni Bw. Anslem Peter.

 Naibu Wazuiri Mavunde, akizungumza mbele ya viongozi wa Hospitali ya Kolandoto mjini Shinyanga.
 Manaibu Waziri Biteko, na Mavunde wakitoka mgodi wa Al-Hilal baada ya ziara yao ya ghafla.
Mwanasheria wa WCF, Bw. Deo Ngoi, (kushoto), akimsimamia Afisa Mwajiri wa Hospitali ya Kolandoto kujaza fomu za kujisajili na Mfuko huo.


SERIKALI YAOMBWA KUENDELEA KUTENGA BAJETI KWA AJILI YA WANAWAKE NCHINI

 Mbunge wa Jimbo la Hanang, Dk.Mary Nagu, akihutubia wakati akifungua akifungua Kongamano la Wanawake na Uongozi 2018 katika Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam jana.
 Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TGNP Mtandao, Vicensia Shule akizungumza kwenye kongamano hilo.
 Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP Mtandao Lilian Liundi akihutubia.
 Profesa Bernadeta Killian akitoa mada kuhusu hali halisi ya wanawake na uongozi hapa nchini.
 Spika wa Bunge Mstaafu Mama Anna Makinda na Naibu Waziri wa Walemavu (Wizara ya Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu) – Stella Ikupa wakiwa kwenye kongamano hilo.
 Wadau mbalimbali wakiwa kwenye kongamano hilo.
 Mbunge wa Jimbo la Hanang, Dk.Mary Nagu (katikati), akiwa na wadau wengine kwenye kongamano hilo.
 Kongamano likiendelea.
 Taswira ya ukumbi kwenye kongamano hilo.


Mbunge wa Bunda, Esther Bulaya akizungumza na wanahabari

Na Dotto Mwaibale

SERIKALI imeombwa kuendelea kutenga bajeti kubwa katika bajeti zake kwa ajili ya kumuendeleza mwanamke wa Tanzania.

Ombi hilo limetolewa na Mbunge wa Jimbo la Hanang, Dk.Mary Nagu wakati akifungua Kongamano la Wanawake na Uongozi 2018 jijini Dar es Salaam jana.

"Tunaomba bajeti ya serikali ibadilike kwa kuangalia ajenda ya jinsia ukizingatia changamoto mbalimbali walizonazo wanawake" alisema Dk.Nagu ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye kongamano hilo.

Dk. Nagu aliwataka wanawake wote kuungana na kuwa kitu kimoja ili kuzijua changamoto walizonazo na kuzitatua kwa msaada wa viongozi wanawake wastaafu.

Aliongeza kuwa wanawake ni jeshi kubwa na ndio wazalishaji wakubwa wa mali
lakini kwa namna moja hama nyingine wamekuwa na changamoto nyingi ikiwemo ya mali zinazotokana na uzalishaji wao kutumiwa na wanaume wao.

Katika hatua nyingine Dk.Nagu aliomba wake wa maraisi wawe mbele kuwaendeleza wanawake wenzao kama ilivyokuwa kwa Mama Anna Mkapa kupitia taasisi yake ya Wote Sawa na Mama Salma Kikwete kupitia WAMA.

Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP Mtandao Lilian Liundi alisema wameamua kuandaa kongamano hilo kama sehemu ya kutoa fursa kwa wanawake na wadau wengine kutafakari wapi wamefanikiwa, wapi bado kama kunachangamoto na kupanga mikakati ya kuimarisha ushiriki wa wanawake katika ngazi zote za maamuzi pamoja na uongozi.

Alisema kongamano hilo pia litatoa fursa ya kutafakari suala la ushauri, ulezi au ukungwi katika kuimarisha uongozi.

Alisema tafiti zinaonesha kuwa nchi za Afrika zinapoteza takribani dola za kimarekani 105 milioni kwa mwaka kwa kutowaingiza wanawake katika uchumi, pia takwimu zinaonesha kuwa wanawake ni zaidi ya asilimia 70 ya wakulima wadogo ambao ndio wanalisha nchi yetu.

Alisema wanawake walioko katika sekta isiyo rasmi ni asilimia 51.1. ambapo wanaume ni 48.9 na kuwa ni asilimia 20 tu ya wanawake ndio wanamiliki ardhi.

Katika kongamano hilo walihudhuria viongozi mbalimbali wa serikali na wadau wengine ambapo kauli mbiu ilikuwa ni "kusherehekea na kutambua Mchango wa Uongozi wa Wanawake Jukwaani na Nyuma ya Pazia".

Mbunge wa Bunda, Esther Bulaya amewataka wanawake kuwa na moyo wa kuthubutu kugombea nafasi mbalimbali za uongozi kwani wanauwezo wa kuongoza.

February 27, 2018

MO Dewji aahidi kuongeza idadi ya wanafunzi wanaopata ufadhili wa taasisi yake


Mwanzilishi wa Taasisi ya Mo Dewji, Mohammed Dewji akikabidhi zawadi kwa baadhi ya wanafunzi wa elimu ya juu waliopata ufadhili kutoka katika taasisi hiyo kwa mwaka wa masomo 2017/2018 kupitia mpango wa Mo Scholars.

Taasisi ya Mo Dewji imetangaza orodha ya wanafunzi 22 wa elimu ya juu waliopata ufadhili kutoka katika taasisi hiyo kwa mwaka wa masomo 2017/2018 kupitia mpango wa Mo Scholars. Wanafunzi hao ni Neema Charles, Winfrida Mrope, Henritha Rwegasira, Monica Ubushimbali, Suzana Mkindi, Hamisa Selemani, Beatrice Shupa, Phoebe Mwankemwa, Amon Abraham, Venance Makambe na Amos Ntandu. Wengine ni Benjamin Mkondya, Ally Mashaka, Amuniri Sebarua, Iddi Mbilinyi, Samwel Ponda, Eram Temu, Busumilo Tumaini, Cosmadeus Mayunga, Amos Kashinje, Kelvin Ernest na Barnaba Barnaba ambao wote ni wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM). Akizungumza kuhusu ufadhili huo, Mwanzilishi wa Taasisi ya Mo Dewji, Mohammed Dewji aliwapongeza washindi kwa kufanikiwa kupata ufadhili huo, lakini akiwataka kujituma ili waweze kufikia malengo waliyojiwekea katika maisha yao.
Mohammed Dewji akizungumza na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambao wanafadhiliwa na Taasisi ya Mo Dewji (hawapo kwenye picha) katika hafla ya kutangaza washindi wa mpango wa ufadhili kwa wanafunzi wa elimu ya juu (Mo Scholars). Picha zote na Rabi Hume.

“Mmepata ufadhili huu muutumie vizuri, wapo wengi ambao walituma maombi lakini nyie mmefanikiwa kupata ufadhili. Msome kwa bidii na baadae mpate kazi nzuri ambazo zitawasaidia kupata kipato na kusaidia ukuaji wa uchumi wa nchi,” alisema Dewji. Dewji alisema aliamua kuanza kutoa ufadhili kwa wanafunzi wa elimu ya juu ili kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli ya kuhakikisha kila mtoto anapata elimu.
Mohammed Dewji akizungumza na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambao wanafadhiliwa na Taasisi ya Mo Dewji katika hafla ya kutangaza washindi wa mpango wa ufadhili kwa wanafunzi wa elimu ya juu (Mo Scholars).

Aliongeza kuwa, dhamira yake ni kuona Watanzania wengi wananufaika na mpango huo na amejipanga kuhakikisha kuwa idadi ya wanufaika wa mpango wa ufadhili unaotolewa na taasisi yake unaongezeka kila mwaka. “Kasi yetu bado ni ndogo sana kulinganisha na ninavyotaka. Wakati tunaanza kutoa ufadhili tuliamua kuanza na wanafunzi 10 lakini mimi nataka tuwape ufadhili Watanzania wengi ikiwezekana tufike hata 100. Kwangu ni jambo jema sana kusaidia Watanzania wenzangu kwa sababu nimezaliwa hapa na nitazikwa hapa sina pengine pa kwenda,” alisema Dewji.
Mmoja wa wanafunzi ambaye kabla ya kupata ufadhili aliweka tangazo kwenye mtandao wa kijamii kwamba anauza figo yake, Amos Ntandu akielezea histori ya maisha yake hadi alilopata ufadhili wa Taasisi ya Mo Dewji.
Nae mmoja wa wanafunzi ambaye kabla ya kupata ufadhili aliweka tangazo kwenye mtandao wa kijamii kwamba anauza figo yake, Amos Ntandu aliishukuru Taasisi ya Mo Dewji kwa ufadhili ambao imewapatia kwani baadhi yao waliokuwa wamepoteza matumaini ya kuendelea na masomo, lakini pia kuomba uongozi wa taasisi kuendelea kutoa ufadhili kwa Watanzania ili wapate elimu. “Mimi nilikuwa tayari kuweka maisha yangu hatarini kwa kutangaza kuuza figo langu, lakini ufadhili huu mliotupatia umebadili maisha yetu. Idadi ya wanafunzi wanaokosa mkopo ni kubwa hivyo nawaomba muwe na moyo wa kuendelea kuwasaidia ili na wao wafikie ndoto zao,” alisema Ntandu.
Mkuu wa Taasisi ya Mo Dewji, Barbara Gonzalez akizungumza kuhusu mpango wa ufadhili kwa wanafunzi wa elimu ya juu (Mo Scholars).

Pamoja na kutangaza washindi hao, pia taasisi hiyo ilitoa zawadi ya kompyuta mpakato (laptop) kwa wanafunzi wa mwaka wa masomo 2016/2017 ambao inawafadhili waliofanya vizuri katika masomo yao kwa mwaka wa kwanza chuoni. Kwa sasa idadi ya wanafunzi ambao wanapata ufadhili kutoka Taasisi ya Mo Dewji imefikia 30, ambapo kati yao wanafunzi 7 ni wa mwaka wa masomo 2016/2017 na wanafunzi 22 mwaka wa masomo 2017/2018.
Baadhi ya wanufaika wa mpango wa ufadhili kwa wanafunzi wa elimu ya juu (Mo Scholars).
Mwanzilishi wa Taasisi ya Mo Dewji, Mohammed Dewji akikabidhi zawadi ya laptop kwa baadhi ya wanafunzi wa elimu ya juu waliopata ufadhili kutoka katika taasisi hiyo kwa mwaka wa masomo 2016/2017 kupitia mpango wa Mo Scholars.