Tangazo

February 28, 2018

SERIKALI YAOMBWA KUENDELEA KUTENGA BAJETI KWA AJILI YA WANAWAKE NCHINI

 Mbunge wa Jimbo la Hanang, Dk.Mary Nagu, akihutubia wakati akifungua akifungua Kongamano la Wanawake na Uongozi 2018 katika Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam jana.
 Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TGNP Mtandao, Vicensia Shule akizungumza kwenye kongamano hilo.
 Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP Mtandao Lilian Liundi akihutubia.
 Profesa Bernadeta Killian akitoa mada kuhusu hali halisi ya wanawake na uongozi hapa nchini.
 Spika wa Bunge Mstaafu Mama Anna Makinda na Naibu Waziri wa Walemavu (Wizara ya Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu) – Stella Ikupa wakiwa kwenye kongamano hilo.
 Wadau mbalimbali wakiwa kwenye kongamano hilo.
 Mbunge wa Jimbo la Hanang, Dk.Mary Nagu (katikati), akiwa na wadau wengine kwenye kongamano hilo.
 Kongamano likiendelea.
 Taswira ya ukumbi kwenye kongamano hilo.


Mbunge wa Bunda, Esther Bulaya akizungumza na wanahabari

Na Dotto Mwaibale

SERIKALI imeombwa kuendelea kutenga bajeti kubwa katika bajeti zake kwa ajili ya kumuendeleza mwanamke wa Tanzania.

Ombi hilo limetolewa na Mbunge wa Jimbo la Hanang, Dk.Mary Nagu wakati akifungua Kongamano la Wanawake na Uongozi 2018 jijini Dar es Salaam jana.

"Tunaomba bajeti ya serikali ibadilike kwa kuangalia ajenda ya jinsia ukizingatia changamoto mbalimbali walizonazo wanawake" alisema Dk.Nagu ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye kongamano hilo.

Dk. Nagu aliwataka wanawake wote kuungana na kuwa kitu kimoja ili kuzijua changamoto walizonazo na kuzitatua kwa msaada wa viongozi wanawake wastaafu.

Aliongeza kuwa wanawake ni jeshi kubwa na ndio wazalishaji wakubwa wa mali
lakini kwa namna moja hama nyingine wamekuwa na changamoto nyingi ikiwemo ya mali zinazotokana na uzalishaji wao kutumiwa na wanaume wao.

Katika hatua nyingine Dk.Nagu aliomba wake wa maraisi wawe mbele kuwaendeleza wanawake wenzao kama ilivyokuwa kwa Mama Anna Mkapa kupitia taasisi yake ya Wote Sawa na Mama Salma Kikwete kupitia WAMA.

Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP Mtandao Lilian Liundi alisema wameamua kuandaa kongamano hilo kama sehemu ya kutoa fursa kwa wanawake na wadau wengine kutafakari wapi wamefanikiwa, wapi bado kama kunachangamoto na kupanga mikakati ya kuimarisha ushiriki wa wanawake katika ngazi zote za maamuzi pamoja na uongozi.

Alisema kongamano hilo pia litatoa fursa ya kutafakari suala la ushauri, ulezi au ukungwi katika kuimarisha uongozi.

Alisema tafiti zinaonesha kuwa nchi za Afrika zinapoteza takribani dola za kimarekani 105 milioni kwa mwaka kwa kutowaingiza wanawake katika uchumi, pia takwimu zinaonesha kuwa wanawake ni zaidi ya asilimia 70 ya wakulima wadogo ambao ndio wanalisha nchi yetu.

Alisema wanawake walioko katika sekta isiyo rasmi ni asilimia 51.1. ambapo wanaume ni 48.9 na kuwa ni asilimia 20 tu ya wanawake ndio wanamiliki ardhi.

Katika kongamano hilo walihudhuria viongozi mbalimbali wa serikali na wadau wengine ambapo kauli mbiu ilikuwa ni "kusherehekea na kutambua Mchango wa Uongozi wa Wanawake Jukwaani na Nyuma ya Pazia".

Mbunge wa Bunda, Esther Bulaya amewataka wanawake kuwa na moyo wa kuthubutu kugombea nafasi mbalimbali za uongozi kwani wanauwezo wa kuongoza.

No comments: