Tangazo

February 12, 2018

MRADI WA ORIO MUARUBAINI WA TATIZO LA UMEME MKOANI KATAVI

 NA SAMIA CHANDE, KATAVI


Mradi wa Orio uliotekelezwa kwa ushirikiano wa  Serikali ya Uholanzi na Tanzania  kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) umesaidia kujenga kituo cha kuzalisha umeme chenye uwezo wa Megawati 2.5 ambazo zimesaidia  kumaliza tatizo la umeme Wilaya ya  Mpanda na Mkoa wa Katavi kwa ujumla.
Kwa mujibu wa Meneja wa TANESCO Mkoani  Katavi, Mhandisi Julius Sabu, kituo hicho kimesaidia kuboresha hali ya upatikanaji wa umeme Mkoani humo, na kutoa umeme wa uhakika na wenye ubora.

“Kituo hicho kinahudumia Wilaya za Tanganyika, Mpanda mjini, maeneo ya Starlike na Kakese”. Aliainisha Mhandisi Sabu.
Lakini pia Kituo kimepunguza gharama za uzalishaji umeme ukilinganisha na Kituo cha zamani.

Wakaazi wa Wilaya ya Tanganyika wameishukuru Serikali na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kwa kuwaletea umeme kwani umekuwa mkombozi katika shughuli zao za kiuchumi, kama vile kuchomelea, "saloon",  na biashara ya maduka.

“Nawashauri Wananchi wenzangu, sasa ni wakati wa kuchangamkia fursa hii inayotokana na kupata umeme wa uhakika katika kukuza shughuli zetu za kiuchumi.” Alisema Mwananchi mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Maneno Mtogwa mkazi wa Wilaya ya Tanganyika.

Meneja wa TANESCO Mkoa wa Katavi ametoa rai kwa Wananchi wa Wilaya za Tanganyika, Mpanda Mjini, maeneo ya Kakese na Starlike kujitokeza kwa wingi kwenye madawati ya huduma kwa Wateja na Ofisi za TANESCO ili kupatiwa huduma kwani TANESCO imejipanga kuwahudumia Wananchi popote walipo na kwa viwango vya hali ya juu.
 Meneja wa TANESCO Mkoa wa Katavi Mhandisi Julius Sabu kiwa anakagua mashine kwenye kituo cha kuzalisha umeme cha Mpanda mkoani Katavi


 Kituo cha kufua umeme cha Mpanda Mkoani Katavi

Vijana wa Wilaya ya Tanganyika wakiwa wanachomelea mageti

No comments: