Tangazo

March 22, 2015

Redio Times, Valentino Hotel kudhamini mafunzo TASWA



Meneja Mkuu wa Royal Valentino Hotel iliyopo Kariakoo Dar es Salaam, Kapara Hamis (kushoto) akizungumza na waandishi wa habari jana kuhusiana na semina ya waandishi chipukizi wa habari za michezo inayoandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), itakayofanyika Jumatano ijayo. Kulia ni Mkurugenzi wa Redio Times FM, Rehure Nyaulawa ambaye redio yake pamoja na hoteli hiyo ndiyo wadhamini wa semina hiyo. Mwingine ni Makamu Mwenyekiti wa TASWA, Egbert Mkoko. (Na Mpigapicha Maalum).

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Na Mwandishi Wetu

REDIO Times FM ya Dar es Salaam imejitokeza kuwa mdhamini mkuu wa semina ya waandishi wa habari za michezo chipukizi  itakayafanyika Jumatano wiki ijayo.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), Egbert Mkoko alimkshukuru Mkurugenzi Mkuu wa Redio Times FM, Rehure Nyaulawa na Meneja wa Valentino Royal Hotel, Kapara Hamis kwa kukubali kugharamia semina hiyo ya siku moja.

“Naomba nitamke kuwa Redio Times FM ndiyo wadhamini wa semina yetu ya siku moja itakayoshirikisha waandishi wa habari za michezo chipukizi, ambapo Valentino Royal Hotel pia ya Dar es Salaam watakuwa wadhamini washiriki wa semina yetu, ambayo itafanyikia hotelini kwao,” alisema Mkoko.

Aliwashukuru wadhamini hao kwa moyo wa kujitolea na kuiomba pia hoteli hiyo iliyopo Kariakoo, Dar es Salaam kuendelea kuipa ushirikiano TASWA na wanamichezo kwa ujumla katika masuala mbalimbali ya udhamini.

Mkoko alisema siku zote chama chake kimekuwa kikipigania kuandaa mafunzo kwa wanahabari wa michezo kama sehemu mojawapo ya kukuza weledi na kwamba wana matumaini Aprili watafanya nyingine kama hiyo na pia Mei mwaka huu watafanya nyingine.

Alisema wataalamu wa michezo mbalimbali kama vile soka, riadha, netiboli, kikapu watapata fursa ya kutoa mada kuhusiana na michezo yao, ambapo pia waandishi wa habari za michezo waliobobea wameitwa kuwaweka sawa chipukizihao, ambao wameteuliwa kutokana na mapendekezo ya wahariri wa habari za michezo wa vyombo husika.

 “Hii ni awamu ya kwanza kwa waandishi wachanga na baadhi ya wa kada ya kati ambao jumla yao ni 40, baada ya hapo tutaendesha mafunzo ya namna hii kwa waandishi waandamizi na wahariri wa habari za michezo.

“Tunaamini baada ya hapo kutakuwa na mabadiliko ya namna fulani, kwani watu tuliowaandaa nina hakika washiriki watashiba vizuri,” alisema na kuongeza kuwa pia kutakuwa na mtoa mada kutoka Shule Kuu ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma (SJMC) ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

Kwa upande wake Nyaulawa alisema redio yake ikiwa ni mdau mkubwa wa habari na michezo kwa ujumla amekuwa akipigania mafunzo kwa wanahabari wa michezo kama sehemu mojawapo ya kukuza weledi.

“Tunaamini waandishi wanapoboresha uandishi wao inachangia kwa kiasi kikubwa kukuza heshima ya vombo vya habari, hivyo tunaomba wadau mbalimbali washirikiane na TASWA inapoandaa mambo kama haya, sisi tumeanza na wengine wasaidie,” alisema.

Naye Kapara wa Valentino Royal, alisema hoteli yake imekuwa ikitumiwa pia na timu mbalimbali zinapotoka nje ya nchi kufikia hapo, hivyo kwa namna ya pekee waandishi wa habari za michezo ni wadau wao, ndiyo sababu hawakusita kukubali kudhamini mafunzo hayo.

No comments: