Tangazo

October 14, 2016

TAARIFA YA NAIBU WAZIRI STELLA MANYANYA KUHUSU VIGEZO VYA UTOAJI WA MIKOPO YA ELIMU YA JUU MWAKA 2016-17


Serikali kupitia Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu, imekuwa ikiwakopesha wanafunzi wenye sifa za kujiunga na vyuo vya elimu ya juu nchini kugharimia masomo yao. Katika utekelezaji wa jukumu hili, Serikali huandaa Sifa na Vigezo vya Utoaji Mikopo kila mwaka ili kuendana na malengo na matarajio yaliyopo katika mipango na mikakati ya kitaifa kama ilivyoainishwa  katika Dira ya Taifa 2025, Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2016/17 -2020/21), Sera ya Elimu na Mafunzo (2014) na Ilani ya Chama cha Mapinduzi. 

Kwa kuzingatia mipango mikakati na sera hizo, pia Mwongozo wa utoaji mikopo kwa mwaka 2016/2017 katika mwaka wa masomo 2016/17, Serikali imetoa vigezo vitakavyozingatiwa katika utoaji mikopo kama ifuatavyo:
 
(i)    Vipaumbele vya kitaifa vinayoendana na mpango wa maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na mafunzo ambayo yatazalisha watalaamu wanaokidhi mahitaji ya kitaifa katika fani za kipaumbele kama vile:

·         Fani za Sayansi za Tiba na Afya,
·         
Ualimu wa Sayansi na Hisabati, 
·         
Uhandisi wa Viwanda, Kilimo, Mifugo, Mafuta na Gesi Asilia
·         
Sayansi Asilia na Mabadiliko ya Tabianchi
·         
Sayansi za Ardhi, Usanifu Majengo na Miundombinu


       (ii)  Uhitaji wa waombaji hususani wenye mahitaji maalum kama vile Ulemavu na Uyatima

       (iii)   Ufaulu wa waombaji katika maeneo ya vipaumbele na umahiri

Kwa hivi sasa Bodi imekamilisha uchambuzi wa majina ya waombaji ambao wana sifa zilizoainishwa hapo juu na majina ya wanufaika wapya yatatangazwa leo tarehe 14 Oktoba, 2016.   Aidha, kuanzia mwaka huu wa masomo, wanufaika wote wa mikopo (wapya na wanaoendelea na masomo) watakopeshwa kulingana na uwezo wao (means tested) katika vipengele vyote vya mikopo.


Imetolewa na:

Mhandisi Stella M. Manyanya (Mb)
NAIBU WAZIRI
ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA
Oktoba 14, 2016

No comments: