Tangazo

February 9, 2018

SIDO YATANGAZA VITA NA WADAIWA WAKE SUGU

Meneja wa Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) mkoa wa Dar es Salaam Macdonald Maganga akitoa uamuzi wa wao kuwaweka kampuni ya udalali ya Yono Auction kwa ajili ya kwenda kukamata wadaiwa sugu wote.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya udalali ya Yono Auction Mart, Scholastica Kevela akitoa tamko la siku 14 kwa wadaiwa sugu wa Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO), kulipa madeni yao kabla ya chukuliwa hatua za kisheria ikiwamo mali zao kupigwa mnada kufidia deni.
Meneja wa SIDO mkoa wa Dar es Salaam Macdonald Maganga akiongoza wafanyakazi na viongozi wa Yono kupita mlango kwa mlango wakati wakizundua kampeni ya kudai madeni "LIPA DENI LAKO SIDO, KUWA MZALENDO'.
 Wakiingia katika moja ya ofisi za mdaiwa wa SIDO.
Nae Mwenyekiti wa Kuatamia mawazo ya wabunifu, Joseph Mlay ameiunga mkono SIDO kwa hatua waliyochukua ya kuingia mlango kwa mlango katika kudai madeni yao. 

 Na Cathbert Kajuna - Kajunason/MMG.

 Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO), mkoa wa Dar es Salaam imetangaza vita kwa wale wadaiwa sugu kulipa madeni yao kabla ya chukuliwa hatua za kisheria ikiwamo mali zao kupigwa mnada. Kauli hiyo ameitoa leo jijini Dar es Salaam, Meneja wa Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO), mkoa wa Dar es Salaam Macdonald Maganga wakati akizindua kampeni ya kukusanya madeni kwa wateja wao. 

 "Leo tunazindua kampeni ya kukusanya madeni kwa wadaiwa sugu wote wa SIDO hatutakuwa na huruma juu ya hili maana hawa ndiyo wanarudisha maendeleo ya shirika nyuma, kuna waliokopa, walipanga kama haujalipa deni lako ujue tunakupa siku 14 tu baada ya hapo sheria itachukua mkondo wake," amesema Mkurugenzi Maganga. 

 Meneja Macdonald Maganga amesema wadaiwa ni wale waliopewa maeneo maalumu ya viwanda kwa ajili ya kufanyia kazi zao na waliopatiwa huduma ya fedha kwa mkopo na kushindwa kurejesha kwa wakati. “Kuna ambao wamekaa miaka mingi au miezi mingi bila kurejesha fedha kwetu kama shirika inatuathiri kwa sababu hatuwezi kuwahudumia wengine,” amesema Maganga. 

 Maganga amesema wanadai jumla ya sh. milioni 350 kutoka kwa wadaiwa zaidi ya 77. 

 Kwa upande wa Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya udalali ya Yono Auction Mart, Scholastica Kevela amewashukuru SIDO kwa kuweza kuwapa kazi hiyo ya kuwakusanyia madeni na kuongeza kuwa hawata muonea huruma mdaiwa yeyote. "Yono Auction Mart tunatoa siku 14 kwa wadaiwa sugu wa Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO), kulipa madeni yao kabla ya chukuliwa hatua za kisheria ikiwamo mali zao kupigwa mnada kufidia deni,". amesema Mama Kevela.

 “Kwa wadaiwa wote wa SIDO, wanaoishi kwenye viwanda na nyumba za SIDO bila kulipa pango, waliochukua mikopo na hawataki kurejesha kwa sababu wanazozijua wao, mkono wa Yono uko kazini ni vyema wakachukua hatua wakalipa ili kuondosha usumbufu,” amesema Kevela.

Mdaiwa Masoud amedai hawafanyi makusudi kutolipa madeni ni kutokana na kodi kupanda kila mwaka huku hali ya biashara ikiwa mbaya. “Ukizingitia soko la ushidani na hali ya bidhaa unashindwa kuuza kwa wakati kwa hiyo tunalipa lakini hatulipi kwa wakati,” amesema.

Amedai wamepangishwa kwa zaidi ya miaka 40 wakifanya shughuli zao na kama wangekuwa hawalipi kwa kipindi chote wangefukuzwa hivyo ameiomba serikali kutodhani kuwa wanapuuza kulipa madeni.

No comments: