Tangazo

March 27, 2018

WAAJIRI WANAWAJIBIKA KISHERIA KUFANYA TATHMINI YA MAJANGA (RISK ASSESSMENT) MAHALAPA KAZI KILA MWAKA-WCF


Mkurugenzi wa Huduma za Tiba na Tathmini, Mfuko wa Fidia Kwa Wafanyakazi,(WCF), Dkt. Abdulsalaam Omar, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko huo, Bw. Masha Mshomba, akitoa hotuba ya ufunguzi wa semina ya siku moja iliyowaleta pamoja mameneja na maafisa waajiri jijini Mwanza ili kupata elimu juu ya umuhimu wa kuzingatia kanuni za Usalama na afya mahala pa kazi ili kumlinda mfanyakazi na madhara yatokanayo na mazingira duni ya kufanyia kazi. Semina hiyo imefanyika jijini humo leo Machi 27, 2018 na kuhudhuriwa na washiriki zaidi ya 200 kutoka wilaya zote za mkoa wa Mwanza. Katikati ni Meneja Tathmini ya Usalama na Afya mahala pa Kazi wa Mfuko huo, Bi. Naanjela Msangi, ambaye idara yake ndiyo imeandaa semina hiyo.
NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID-MWANZA
TATHMINI ya majanga (risk assessment), mahala pa kazi inapaswa kufanywa kila mwaka kwa mujibu wa sheria, Meneja Tathmini za Usala na Afya mahala pa kazi wa Mfuko wa Fidia Kwa Wafanyakazi, (WCF), Bi. Naanjela Msangi amesema.
Bi. Msangi ameyasema hayo wakati akiwasilisha mada kuhusu tathmini ya majanga (Risk Assessment) kwenye viwanda na maofisini wakati wa semina ya mafunzo kwa Mameneja na Maafisa Waajiri waandamizi kutoka sekta ya umma na binafsi jijini Mwanza, Machi 27, 2018.
“Sheria inatamka kiwanda au ofisi yoyote ile inapaswa kufanya tathmini kabla ya kuanza uzalishaji, majanga haya yanaweza kutokea wakati tayari uko kwenye operations,(uendeshaji) sasa ni vema uanze kufanya risk assessment kabla ya kuanza uzalishaji.” Alifafanua.
Akizungumzia sababu za kufanya tathmini kila mwaka, Meneja huyo alisema, yawezekana kiwanda au ofisi kubadilisha njia ya uzalishaji kutoka ilivyokuwa awali hivyo itasaidia kujua vile viwango vya hatari ya kutokea majanga vimeongezeka au la ili uchukue hatua za kujikinga na kutokea kwa majanga mahala pa kazi.
Akifungua semina hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Bw. Masha Mshomba, Mkurugenzi wa Huduma za Tiba na Tathmini wa Mfuko wa Fidia Kwa Wafanyakazi, (WCF), Dkt. Abdulsalaam Omar, aliwaasa waajiri kuzingatia sheria na mahusiano mahala pa kazi ambayo pamoja na mambo mengine inamtaka mwajiri kuhakikisha wafanyakazi wake wanafanya kazi katika mazingira salama, kwa kuwapatia vifaa vya kujikinga na majanga (Personal Protective equipments).
“Pamoja na wajibu wetu wa msingi wa kusajili waajiri na kuhakikisha wanawasilisha michango ya kila mwezi kwa ajili ya wafanyakazi wao, ili panapotokea ajali, kuumia au kifo mahala pa kazi na hatimaye Mfuko kuchukua jukumu la kulipa Fidia kwa muathirika au wategemezi wake,  lakini pia tunalojukumu la kuzuia majanga yasitokee mahala pa kazi kwa kutoa elimu na ndiyo lengo mahsusi la semina hii ya leo.” Alisema Dkt. Omar.
Alisema, dhumuni lingine la semina hiyo ni kuzungumzia masuala muhimu kuhusu Mfuko kupitia mada mbalimbali zitakazowasilishwa na wataalamu wa WCF na masuala hayo n I pamoja na kuhamasisha na kusisitiza wafanyakazi kuzingatia kanuni za kulinda na kudumisha usalama na afya mahala pa kazi na masuala ya Fidia kwa Wafanyakazi wanaoumia, kuugua au kufariki kutokana na kazi.
“Vile vile ni kuelimisha haki na wajibu wa mwajiri na mwajiriwa katika kuwezesha Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi kushughulikia kwa ufanisi madai ya Fidia kwa Wafanyakazi.” Alifafanua.
Kwa ufupi niseme tu kwamba Mfuko una faida kubwa kwa Wafanyakazi, Waajiri na Taifa kwa ujumla kwani hivi sasa wafanyakazi wanauhakika wa kinga ya kipato kutokana na majanga yasababishwayo na ajali, magonjwa au vifo kutokana na kazi, alisema Dkt. Omar.
Mmmoja wa washiriki wa semina hiyo Bi.Asmini Gombo, ambaye ni Meneja Rasilimali watu wa kampuni ya Mincom Rockdrills Tanzania Limited, alisema wao kama kampuni swala la kufanya tathmini ya majanga mahala pa kazi lina umuhimu mkubwa kwani sio tu linakusaidia kutambua ni vitu gani ambavyo kampuni inaweza kuboresha ili kuepuka majanga lakini pia inasaidia kudumisha usalama na afya za wafanyakazi. 

“Sisi huwa tunafanya tathmini kila baada ya miezi mitatu na hii imekuwa ikitusaidia sana kuhakikisha usalama wa wafanyakazi wetu unazingatiwa na nitoe rai tu kwa wenzangu wajenge ratiba ya kufanya zoezi hili si lazima iwe kila baada ya miezi mitatu kama tunavyofanya sisi lakini hata kila baada ya miezi sita kwani utapunguza majanga na hivyo kuokoa rasilimali watu na mali za kampuni pia." Alisema.

Pia alisipongeza WCF kwa kutoa elimu kwani awali walijua kazi kubwa ya Mfuko ni kusajili na kukusanya michango kutoka kwa waajiri kumbe pia inao wajibu wa kuelimisha waajiri kuepukana na majanga yanayoweza kutokea sehemu za kazi.
Asmini Gombo, Meneja Rasilimali watu wa kampuni ya Mincom Rockdrills Tanzania Limited, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu elimu aliyopata kutokana na semina hiyo.

Washiriki wakisikiliza hotuba ya mgeni rasmi, Dkt. Omar.
Washiriki wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa semina.
Mshiriki akisoma kijarida chenye maelezo yahusuyo shughuli za Mfuko.
Mkurugenzi wa Huduma za Tiba na Tathmini, Mfuko wa Fidia Kwa Wafanyakazi, Dkt. Abdulsalaam Omar, (kushoto), Meneja Tathmini ya Usalama na Afya mahala pa Kazi wa Mfuko huo, Bi. Naanjela Msangi, (kulia), na Afisa Matekelezo wa Mfuko huo, Bw. George Faustine, wakiwa tayari kuanza kwa se mina hiyo.
Afisa Matekelezo wa Mfuko huo, Bw. George Faustine, akitoa mada juu ya wajibu wa mwajiri kutekeleza sharia iliyoanzisha Mfuko wa Fidia Kwa Wafanyakazi. ambapo alizungumzia wajibu wa mwajiri kujnisajili na Mfuko, kupeleka michango kila mwezi, na kutoa taarifa za wafanyakazi wake kwa usahihi.
Washiriki wakisikiliza hotuba ya mgeni rasmi, Dkt. Omar.

Washiriki kwa umakini wakifuatilia mada zilizokuwa zikiwasilishwa na wataalamu wa WCF.
Bi. Naanjela Msangi

Baadhi ya washiriki wakifuatilia mada zilizokuwa zikiwasilishwa na wataalamu wa WCF jijini Mwanza Machi 27, 2018.
Dkt. Abdulsalaam(kushoto), akibadilishana mawazo na baadhi ya washiriki mwishoni mwa semina.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, (WCF), Bi. Laura Kunenge, (katikati), na Robert Duguza, (kushoto), Afisa wa usalama na afya mahala pa kazi wa Mfuko huo, wakimsikiliza mmoja wa washiriki ambaye alihitaji ufafanuzi Zaidi kuhusu masuala mbalimbali yahusuyo Mfuko huo mwishoni mwa semina.
Meneja Tathmini za Usalama na Afya mahala pa kazi wa Mfuko huo, Bi. Naanjela Msangi(kushoto), akimsikiliza mmoja wa washiriki aliyehitaji ufafanuazi Zaidi wa masuala yaliyozungumzwa kwenye semina hiyo.
Mkurugenzi wa Huduma za Tiba na Tathmini, Mfuko wa Fidia Kwa Wafanyakazi, (WCF), Dkt. Abdulsalaam Omar (mwenye tai) na Meneja Tathmini za Usala na Afya mahala pa kazi wa Mfuko huo, Bi. Naanjela Msangi (wapili kulia), wakisikiliza hoja mbalimbali za washiriki wa semina mara baada ya kumalizika kwake.
Afisa Matekelezo (Compliance Officer), wa Mfuko wa Fidia Kwa Wafanyakazi, (WCF), Bw. George Faustine(mwenye tai), akifafanua masuala mbalimbali kwa washiriki mwishoni mwa semina hiyo.
Sehemu ya picha ya pamoja ya washiriki.

No comments: