Tangazo

August 2, 2012

Wazo la Mdau Kuhusu Tuzo za VODACOM

August 01, 2012, Mbeya,

Awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kuwapongeza kwa dhati kabisa washindi wa tuzo za kwanza za umahiri wa dijitali zilizoandaliwa na kampuni ya simu za mikononi ya Vodacom, nchini Tanzania (The Vodacom Awards for Digital Excellence – VADE). Na kwa upekee kabisa, napenda niwataje washindi hao ambao ni wafuatao:

Mikocheni Report, Issa Michuzi, Wanamuziki Tanzania, Kipanya.co.tz, Vijana FM, Millardayo.com, Taste of Tanzania, Jamii Forums, Mambo Magazine pamoja na DJ Fetty Blog.

Toka kutangazwa kwao, msimamo wangu umekuwa ni kwamba, sina tatizo na washindi, maana mwisho wa siku naamini hawakujichagua wao wenyewe. Lakini niongeze pia kuwa, huenda sina tatizo na waliowachagua washindi hao, kwani ni wazi walichagua washindi kulingana na vigezo ambavyo viliwekwa na ndio maana waandaaji hawakuwa na lolote la kusema pindi walipotajwa washindi hao, zaidi ya kuwapa tuzo zao.

Na baada ya hapo, bilashaka sasa ninabakia na upande ambao nina matatizo nao. Upande wa waandaaji wa tuzo hizi, na hapa nikimaanisha kampuni ya simu za mikononi ya Vodacom.

Kwangu mimi, utoaji wa tuzo hizi, umekuwa ni mwendelezo wa usanii ambao umekuwa ukifanywa na kampuni hii katika kuhakikisha kuwa wanatumia udhaifu wa kisheria, weledi na mshikamano baina ya waandishi wa habari wa mtandaoni, kujinufaisha zaidi wao badala ya kuwanufaisha wanahabari hawa ambao ni wazi wamekuwa wakiwafanyia kazi kubwa sana.

Yapo mambo kadhaa ambayo binafsi nimeyaona kuwa ni usanii mkubwa sana ambao umefanywa na Vodacom hapa na wala haikuwa kwa lengo la kuinua wahusika au tasnia ya uandishi wa mtandaoni kwa ujumla wake na miongoni mwayo ni pamoja na vigezo ambayo vilitumika katika utoaji wa tuzo hizo.

1. kati ya vigezo ambavyo nilisikia kuwa walivitumia, ni pamoja na blog au blogger husika kuwa na blog ambayo habari anazoziweka hazitokani na kutafsiri kutoka mitandao yoyote ile iwe ya ndani au nje ya nchi wala kuwa imechukuliwa toka blog zingine.

Miongoni mwa blog ambazo zilishinda kama ambavyo nimezitaja hapo juu, zipo ambazo zimekuwa zikiandika kazi za wasanii wa nje ambazo wenyewe wamekuwa wakitamka kabisa maneno “…kwa mujibu wa mtandao fulani, redio fulani, jarida fulani nk” Je, Vodacom hawakuliona hili kuwa ni kinyume na vigezo vyao hapo?

2. Nimesoma mahali kuwa Vodacom waliliasisi wazo hili mwezi uliopita, kwa maana ya mwezi Julai mwaka huu, ingawa linaelezwa pia kuwa lilikuwa wazo la muda mrefu na kisha mwezi huo huo tuzo hizo zikatolewa.
Je, Vodacom wanaweza kutusaidia kujua ni jinsi gani waliwashirikisha blogger katika kuandaa tuzo zenyewe, kwa maana ya kuweka vigezo, sababu ya vigezo hivyo, mechanism ya kuhakikisha kuwa vigezo vinafuatiliwa (hasa linapokuja suala la takwimu), na mambo mengine ya namna hiyo?

3. Katika kuangalia kile walichosema kuwa habari kwenye hizo blog zinatakiwa ziwe zimeandikwa na mtu mwenye ujuzi nazo, je walikuwa na mechanism gani pia katika kuhakikisha hili? Maana Vodacom ni kampuni ya simu, haina wataalamu wala weledi wa masuala ya habari.

Upo uwezekano mkubwa sana kuwa walitumia kitengo chao cha mawasiliano na umma au kitengo chao cha habari nk, (kulingana na wanavyokiita wao), lakini pia upo ukweli wa wazi kuwa kitengo hiki sawa na kile cha masoko, vimekuwa vitengo vyenye kuonyesha waziwazi udhaifu wao katika utendaji kazi wao kiasi cha kuzua maswali miongoni mwa wenye kuvifuatilia.

Hebu tujiulize, si hawa hawa Vodacom ambao walizua mjadala mkubwa sana baada ya kuwa miongoni mwa wadhamini wa blog ambayo ilikuwa ikitajwa kuwa imejaa matusi mengine ambayo hayafai hata kusimuliwa mbele za watu waliostaarabika? Watu wa habari kama wapo, na kama walishindwa kubaini mapungufu ya kilichokuwa kimejaa katikablog hiyo, leo hii wanawezaje kutushawishi kuwa walikuwa bora katika kuibua na kutekeleza wazo la VADE? Na wale wa masoko nao halikadhalika?

Je, Vodacom kweli walishindwa kuwa waungwana walau hata kushirikisha waasisi wa fani hii katika Tanzania, wakiwemo akina Ndesanjo Macha, Jeff, na wengineo ambao tunawajua kuwa bila wao leo hii Watanzania bado tungekuwa tunasikia tu kitu blog katika vyombo vya habari?

Ni aibu sana kwa kampuni kubwa kama hii kuchukulia suala la tuzo kama mechi fulani ya wanywapombe wanaoamua kujifurahisha katika kile wanachokipachika jina la Bonanza. Aibu kwasababu, hata utoaji wa tuzo wenyewe, lilikuwa tukio ambalo lilikuwa jepesi jepesi mno. Halikuwa na mwamko wa namna hiyo, na pengine ni kutokana na ukweli kuwa wenyewe walishajua kuwa wamefanya madudu kwahiyo ili kuepuka aibu, basi wasiifanye kuwa issue kubwa.

Na ni katika muktadha huu basi ambako binafsi najiuliza, Je, Vodacom, wameona kuwa kilicho cha muhimu kwao ni kujitangaza tu bila hata kujali kuwa kujitangaza kwenyewe kunahusisha kuwa watupu? Lakini pia nageuka upande wa waandishi wa habari hususan ambao wamezitwaa tuzo hizo.

Mmejisikiaje kupata kitu ambacho kama wana taaluma mnaelewa wazi na nafsi zenu zinawaeleza kuwa mmefanywa kombe lililofunikwa ili mwanaharamu fulani apite na aendelee na hamsini zake?

Inawezekana kabisa kuwa wazo lilikuwa zuri, na hakika ninaafiki sio tu kuwa wazo lilikuwa zuri, bali lilikuwa zuri sana, lakini utekelezwaji wa wazo hili, umekuwa ni tukio la aibu ambalo binafsi ninaamini kabisa kuwa Vodacom, watatakiwa kukaa na kujitathmini juu ya namna wanavyowatumia waandishi wa habari.

Ni hadi pale tutakapofikia mahali pa kutambuana na kuthaminiana ndipo tutaweza kusonga mbele kimaendeleo, kinyume na hapo, hii tabia ya wengine kuwa wanyonge na wengine kuwa mahiri katika kutumia udhaifu wa wengine kitaaluma, kiumoja na hata kiueledi, itafikia mahali itatuumbua hadharani kweupeeeeee!! Kama ambavyo imeshaanza kujionyesha sasa ambapo nasikia kuwa mmoja wa washindi, ambaye ni Michuzi, amerejesha tuzo hiyo kwa waandaaji. Sijui kwa kuikataa, kuona haimstahili anataka wambadilishie wampe nyingine au vipi.

Niko tayari kukosolewa pale ambapo siko sahihi
Ramadhan Msangi
CEO – Jukwaa Huru Media

No comments: