Tangazo

September 1, 2014

MRADI WA MAJARIBIO WA KUFUNDISHA MASOMO YA SAYANSI WA UNESCO WANEEMESHA TANZANIA

DSC_0018
Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) Tanzania, Zulmira Rodrigues akisoma risala ya kufungwa kwa mradi huo ambao uliojulikana kama Micro Science Kits (MSKs) kwa wadau wa elimu, wakuu wa shule mbalimbali, maafisa elimu na maofisa wa serikali kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi za shirika hilo jijini Dar.

Na Mwandishi wetu

MRADI wa miaka minne wa kusaidia ufundishaji wa masomo ya sayansi kwa kufanikisha majaribio ya maabara uliokuwa ukifadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la elimu na sayansi na utamaduni (UNESCO) na kuendeshwa na wizara ya elimu nchini katika shule 180 zilizopo katika wilaya 34 umemalizika kwa mafanikio huku wito ukitolewa kutafutwa njia ya kuendeleza mradi huo.

Tangu awali mradi huo haukuelezwa kinaga ubaga unakuaje endelevu kama utaonekana kuwa na manufaa kwa taifa.

Akitoa maelezo ya kufungwa kwa mradi huo ambao uliojulikana kama Micro Science Kits (MSKs) kwa wadau wa elimu,wataalamu na maofisa wa serikali, Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) Tanzania, Bi. Zulmira Rodrigues aliwataka wadau hao kuzingatia mafanikio yaliyokuwapo,kuangalia changamoto zake na kuona namna ya kuendeleza mazuri ya mradi.

Mradi huo wa majaribio ulifanyika katika shule za mikoa ya Mbeya, Kilimanjaro, Mwanza, Shinyanga, Dodoma, Kagera, Morogoro, Kigoma na Tanga kwa upande wa Tanzania Bara.

Aidha ilielezwa katika kikao hicho kilichofanyika ofisi za Unesco kwa lengo la kuufunga rasmi pamoja na malengo yake ya kuboresha elimu Tanzania kwa kuhakikisha masomo ya sayansi yanafundishwa kwa namna inavyotakiwa, tathmini ilionesha udhaifu wa kutokuwepo na mpango madhubuti wa kuendelezwa kwake.
DSC_0015
Mradi huu wa majaribio wa MSK ulilenga kukuza uwezo wa kufundisha masomo ya sayansi (baiolojia,kemia na fizikia) kwa shule ambazo hazina maabara kwakuzipatia visanduku vya majaribio pia uliendesha warsha mbalimbali ili kukuza uwezo wa matumizi ya zana zilizo katika mradi wa MSK pamoja na vitabu vya kufundishia.

Aidha mradi huo ulizingatia pia kuongeza upendo wa masomo ya sayansi kwa jamii na kuwafanya wanafunzi wapende na wawe na hamu na masomo ya sayansi.

Mradi huo ambao umefanyika kwa kuzingatia pia mahitaji ya taifa na kimataifa chini ya dhana ya kuendeleza masomo ya sayansi duniani unaendeshwa na UNESCO kwa kujenga uwezo wa shule za sekondari na msingi kufanya mazoezi ya utambuzi wa nadharia mbalimbali kimaabara hutoa masanduku maalumu ambayo yanakuwa ni kama maabara ndogo zinazotembea.

Maabara hizi hutoa uwezo wa kufanyika kwa majaribio ya msingi na yale makubwa kwa kuzingatia madaraja mbalimbali ya mafunzo kuanzia ngazi za chini kati na juu.

Katika ufungaji wa mradi huo uliofanyika mwishoni mwa mwezi Agosti washiriki walielezwa maendeleo ya mradi hadi mwisho wake na changamoto zilizokuwa zinakabiliwa.

Unesco imesema kutanuka kwa kasi kwa elimu ya msingi kumesababisha changamoto za ubora wa elimu katika mfumo wa elimu nchini na mradi wa majaribio ulionesha kwamba ubora unaweza kurejeshwa kwa kuwa na mpango kama MSKs.
DSC_0021  
Pichani juu na chini ni baadhi ya wadau wa elimu, wakuu wa shule mbalimbali, maafisa elimu na maofisa wa serikali waliohudhuria mkutano huo uliofanyika mwishoni mwa juma.

Kutokana na changamoto za raslimali kushindwa kuhakikisha kwamba kila darasa, mwalimu na mwanafunzi wanakuwa na zana zinazotakiwa kufundisha na kujifunza,walimu na wanafunzi walielemewa na hivyo kuathiri ufundishaji wa masomo ya sayansi ya baiolojia, kemia na fizikia.

Mathalani matokeo ya kidato cha nne ya mwaka 2011 wastani wa matokeo ya masomo ya sayansi kitaifa uliporomnoka chini ya asilimia 50.

Fizikia ilikuwa aislimia 43.2, kemia 43.3 na baiolojia 43.4 na katika takwimu hizo zilionesha kwamba wasichana walifanya vibaya zaidi.

Utafiti ulionesha wazi kwamba udhaifu huo umetokana na kukosekana kwa maabara, vifaa vya kufundishia na upungufu mkubwa wa walimu wa sayansi.

Pamoja na kuwepo kwa changamoto za uhaba wa masanduku haya ya maabara, tathmini iliyiofanywa ilionesha kwamba mradi ungeliweza kuunganishwa na miradi kama ya JICA na pia kutengenezewa mfumoi wa wa kuweza kuwa endelevu kutokana na umuhimu wake na ufanisi.

Changamoto kama za masanduku machache kuliko yalivyokusudiwa katika mradi , muda mfupi wa kufunza walimu na pia kutekeleza yote yaliyopangwa na suala la ukaguzi bado mradi huu kutokana na asili yake ungelikuwa na maana zaidi kuendelezwa ili kufikia zaidi shule zilizo pembezoni.
DSC_0009
Aidha ili kuendelea na mradi huo tathmini iliyofanywa na kuelezwa na Ellen Binagi katika kikao cha wadau ilishauriwa serikali kufikiria kuanzisha vituo na taasisi za kutengeneza maabara hizo ndogo nchini badala ya kuagiza kutoka nje kutokana na gharama zake na hasa ikizingatiwa kwamba Tanzania ni nchi kubwa na yenye shule nyingi.

Binagi alisema kwamba kuanzishwa kwa mtindo huo kumeleta muonekano mpya katika upenzi wa masomo ya sayansi na katika shule za majaribio ufanisi wake ulikuwa mkubwa na ipo haja ya kuangalia namna ya kuendeleza.

Mtathmini huyo pia amesema ipo haja kwa UNESCO na serikali ya Tanzania pamoja na mradi kumalizika kuona namna ya kuuendeleza na kuondoa changamoto zilizoonekana wakati wa utekelezaji wake.
DSC_0012

No comments: