Tangazo

November 19, 2014

WATOTO 130000 WANAISHI NA MAAMBUKIZI YA VVU



Na Johary Kachwamba-MAELEZO

TAKWIMU zinaonesha kwamba watoto 130000 wana maambukizi ya Virusi Vya UKIMWI (VVU) kati ya hao 39317 wamefikiwa na kupatiwa huduma ya dawa za kupunguza makali ya virusi hivyo. 

Hayo yamesemwa leo na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Dkt. Pindi Chana (pichani) wakati akifungua kongamano la nne la kitaifa la  VVU na UKIMWI kwa watoto linalofanyika  katika Ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere uliopo jijini Dar-es-salaam.

Dkt . Chana alisema asilimia 39 ya watoto walio katika hatari ya kupata maambukii ya  UKIMWI hupimwa vipimo vya kubaini maambukizi ya VVU ndani ya miezi miwili baada ya kuzaliwa hivyo basi kuna  umuhimu kwa watoto hawa kupata huduma za tiba mapema.

Akizungumzia maambukizo ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto waziri huyo alisema Tanzania imepiga hatua katika kuzuia maambukizo kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto lengo likiwa  ni kutokomeza kabisa maambukizi mapya kwa watoto wachanga.

“Mama wajawazito na wale wanaonyoyesha wanapatiwa huduma ya dawa za kupunguza makali ya VVU mara tu wanapogundulika kuwa na maambukizo, kupitia mpango mpya unaojulikana kama ‘uwezekano namba 2 au (Option B+)”, alisema Dkt.Chana.

Alisema  kufikia mwezi Juni mwaka huu  jumla ya akina mama 940900 kati ya 1050043 hii ni sawa na asilimia 89.6% ya waliohudhuria kliniki walipimwa UKIMWI kati ya hao 47856 takribani asilimia 5 walikutwa na  maambukizi ya VVU. 

Kwa upande wa watoto 20569 walipima kipimo cha DBS kati ya hao  2063  hii ni sawa na asilimia 10 walikutwa na maambukizo ya VVU.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Dkt. Donan Mbando, alisema ingawa nchi imepiga hatua katika mapambano ya kudhibiti UKIMWI  hali halisi  inaonyesha  kuwa bado kuna maambukizo yanatokea sio tu kwa watu wazima bali na  kwa watoto pia.

“Ni jukumu letu kuendelea kuweka mikakati ya dhati na kuisimamia ili kuhakikisha lengo la kutokomeza maambukizo ya VVU tunalifikia kwani mwaka 1986 maambukizi yalikuwa juu kwa asailimia 18 lakini hivi sasa yameshuka na kufikia asilimia 5.3”, alisema Dkt. Mbando.

Kwa upande wake  Mkurugenzi wa ufundi kutoka Taasisi ya Elizabeth Glaser Pediatric Aids (EGPAF) ambao ni waandaaji wa kongamano hilo  Chrispin Kimario alisema ni muhimu kwa wazazi na jamii kushirikiana kwa pamoja na kulibeba jukumu la  kuhakikisha kila mama mjamzito anapata huduma ya vipimo husika na matibabu kwa wakati.

Kimario alisema, “Watoto wameachwa nyuma, ni vyema tukumbuke kuwa mtoto hawawezi kujipeleka wenyewe hospitali kupima afya zao, hivyo ni jukumu letu wazazi, walezi na jamii kwa ujumla kuhakikisha watoto hawa wanapata huduma wanazostahili”.

Kauli mbiu ya kongamano hilo la siku mbili ambalo limehudhuriwa na wadau wa afya kutoka asasi za umma na binafsi za ndani na nje ya nchi ni ongeza kasi: Rahisisha upatikanaji wa utumiaji wa huduma za VVU na Ukimwi, pata matokeo chanya ya afya za mama na watoto wanaoishi na VVU.

No comments: