Tangazo

November 25, 2015

SERIKALI YAAHIDI KUSHIRIKIANA NA MASHIRIKA NA WADAU WA HABARI KUTOKOMEZA VITENDO VYA UKATILI KWA WAANDISHI WA HABARI

IMG_2832
Mkuu wa ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues (katikati) akisalimiana na Mjumbe wa bodi udhamini ya Mtandao wa Radio Jamii Tanzania (COMNETA), Balozi Mstaafu, Christopher Liundi alipowasili katika mkutano wa kitaifa wa mashauriano kuhusu hali ya usalama wa waandishi wa habari, uzinduzi wa kikosi kazi cha usalama wa waandishi wa habari na uandishi unaozingatia maadili ulioandaliwa na UNESCO. Kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Prof. Ole Sante Gabriel.

Na Rabi Hume, Modewjiblog

Serikali mpya ya awamu ya tano iliyochini ya rais Dr. John Magufuli, imeahidi kushirikiana na mashirika na wadau mbalimbali ambao wamekuwa wakipambana kuhakikisha waandishi wa habari wanakuwa salama na kufanya kazi zao kwa uhuru bili kuingiliwa ufanyaji wa kazi zao na mtu yoyote.

Ahadi hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Prof. Ole Sante Gabriel katika mkutano wa kitaifa wa mashauriano kuhusu hali ya usalama wa waandishi wa habari, uzinduzi wa kikosi kazi cha usalama wa waandishi wa habari na uandishi unaozingatia maadili ulioandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia na Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Prof. Gabriel amesema serikali ya awamu ya tano ipo tayari kushirikiana na mashirika na wadau mbalimbali ambao wapo kuwasaidia waandishi wa habari ili haki zao ziweze kutekelezwa kutokana na kuwepo kwa uvunjaji wa haki za wanahabari.

Amesema wanatambua kuwepo kwa changamoto hizo kwa waandishi wa habari na kwa serikali ya awamu ya tano itahakikisha kushirikiana na mashirika na wadau ili kutetea haki za wanahabari kwa kuwa na uhuru katika utendaji wa kazi zao bila kuingiliwa na mtu.

“Naahidi kuanzia sasa serikali itakuwa ikishirikiana nanyi kusaidia kuhakikisha kunakuwa na uhuru wa vyombo vya habari, nchi yetu kwa sasa haina sababu ya kuacha kuungana na ninyi kutokomeza vitendo hivyo kwa wanahabari, serikali ni mpya na tutalitekeleza jambo hilo kila tumaposhirikishwa kuhusu vitendo vibaya kwa wanahabari,” amesema Prof. Gabriel.
IMG_2843
Mkuu wa ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues akitoa neno la ufunguzi katika mkutano huo kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi kufungua.

Aidha Katibu Mkuu huyo amewata waandishi wa habari kuwa pamoja na usaidizi ambao wizara imeamua kujitoa kuwasaidia pia wanapaswa kuandika habari zenye weledi na zilizo sahihi kwani kumekuwepo na kundi kubwa la waandishi wa habari ambao wamekuwa wakiandika habari ambazo hazina uhakika wala weledi na hivyo kuupotosha umma kwa habari wanazoandika ila kuanzia sasa wanabidi kubadilika kwa kuandika habari ambazo zitakuwa na fadia kwa jamii inayowazunguka.

Kwa upande wa UNESCO, kupitia kwa Mkuu wa ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues, amesema kumekuwepo na vitendo vingi ambavyo sio vya kibinadamu ambavyo wamekuwa wakifanyiwa waandishi wa habari na wao wameamua kujitoa kuhakikisha wanatokomeza vitendo hivyo.

Amesema kama jamii ikiungana kwa pamoja kutokomeza vitendo hivyo inawezekana kwani kutokuwepo uhuru wa waandishi wa habari katika utendaji wao wa kazi kunapelekea jamii kukosa baadhi ya taarifa muhimu ambazo kama kukipatikana uhuru wa habari kutawapa fursa wanahabari wa kuzitoa taarifa hizo.
IMG_2914
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Prof. Ole Sante Gabriel akisisitiza jambo wakati akifungua rasmi mkutano wa kitaifa wa mashauriano kuhusu hali ya usalama wa waandishi wa habari, uzinduzi wa kikosi kazi cha usalama wa waandishi wa habari na uandishi unaozingatia maadili ambao umeandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na Elimu, Sayansi (UNESCO).

“UNESCO tunapenda kuona vitendo hivyo havifanyiki kwa waandishi wa habari kama kuweka sheria ambazo zinawabana na kusababisha wanashindwa kufanya kazi zao kwa uhuru na tunaweza kuona kama serikali na kila mtu akiwa tayari tunaweza kumaliza tatizo hilo,” amesema Rodrigues.

Nae Makamu wa Rais wa Chama cha Kijamii cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Flaviana Charles amesema imekuwa ngumu kesi zinazokuwa zikiwahusu waandishi wa habari juu ya vitendo vya kikatili wanavyotendewa kutokana na ucheleweshwaji wa upelelezi unaofanywa na Jeshi la Polisi Tanzania akitolea mfano kesi ya mwandishi wa zamani wa Chaneli 10 mkoani Iringa, Daudi Mwangosi ambapo mpaka sasa ina miaka 4 na bado upelelezi haujakamilika.
IMG_3149
Makamu wa Rais wa Chama cha Kijamii cha Wanasheria wa Tanganyika, Bi. Flaviana Charles akifafanua jambo wakati wa mkutano huo.
IMG_2873
Pichani juu na chini ni wahariri wa vyombo vya habari, waandishi wa habari, wadau wa tasnia ya habari pamoja na maafisa wa UNESCO na taasisi mbalimbali walioshiriki mkutano huo.
IMG_2925
IMG_3178
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) katika tasnia ya Habari na Mawasiliano, Ayub Rioba akiwasilisha mada ya wajibu wa vyombo vya habari huku akitolea mfano wa moja ya habari iliyobeba kichwa cha habari "Uhuru wa habari watikiswa Zimbabwe" katika moja ya magazeti ya Serikali wakati wa mkutano wa kitaifa wa mashauriano kuhusu hali ya usalama wa waandishi wa habari, uzinduzi wa kikosi kazi cha usalama wa waandishi wa habari na uandishi unaozingatia maadili ulioandaliwa na UNESCO.
IMG_3115
Ofisa Miradi katika kitengo cha Mawasiliano na Tehama UNESCO, Nancy Kaizilege akiwasilisha mada ya Uhuru wa vyombo vya Habari katika mkutano huo.
IMG_3191
Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Mwanasheria Onesmo Olengurumwa akielezea jinsi mtandao wake unavyotoa msaada kwa wanahabari wanaokumbwa matukio mbalimbali katika utendaji wao hususan msaada wa kisheria.
IMG_3206
Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Tanzania Daima, Neville Meena akiuliza swali kwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Assah Mwambene (hayupo pichani) katika mkutano wa kitaifa wa mashauriano kuhusu hali ya usalama wa waandishi wa habari, uzinduzi wa kikosi kazi cha usalama wa waandishi wa habari na uandishi unaozingatia maadili sambamba na kuadhimisha "International Day to #EndImpunity" ulioandaliwa na UNESCO.
IMG_3212
Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Assah Mwambene akitolea ufafanuzi wa swali la Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Tanzania Daima, Neville Meena (hayupo pichani).
IMG_3227
Mkuu wa ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues akitoa maoni katika katika mkutano wa kitaifa wa mashauriano kuhusu hali ya usalama wa waandishi wa habari, uzinduzi wa kikosi kazi cha usalama wa waandishi wa habari na uandishi unaozingatia maadili sambamba na kuadhimisha "International Day to #EndImpunity" ulioandaliwa na UNESCO.
IMG_3234
Mjumbe wa bodi udhamini ya Mtandao wa Radio Jamii Tanzania (COMNETA), Balozi Mstaafu, Christopher Liundi akitoa pongezi kwa Shirika la UNESCO katika kuhamasisha Amani kupitia, Redio za Jamii, makongamano mbalimbali pamoja na kuwashirikisha viongozi wa dini kuhubiri Amani nchini katika mkutano huo.
IMG_3237
Mwandishi wa habari mkongwe, Halima Sharrif akitoa maoni katika mkutano huo.
IMG_3047
IMG_3069
Kutoka kushoto ni Ofisa miradi katika kitengo cha Mawasiliano na Tehama UNESCO, Nancy Kaizilege, Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Mwanasheria Onesmo Olengurumwa, Mkuu wa ofisi na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Zulmira Rodrigues pamoja na Makamu wa Rais wa Chama cha Kijamii cha Wanasheria wa Tanganyika, Bi. Flaviana Charles katika picha ya ukumbusho.
IMG_3107
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Prof. Ole Sante Gabriel (kushoto) akifurahi jambo na Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Tanzania Daima, Neville Meena mara baada ya zoezi la picha ya pamoja.

No comments: