Tangazo

May 26, 2017

MBEGU BORA ZA MHOGO ZINAHITAJIKA KUWANUSURU WAKULIMA WILAYANI CHATO MKOANI GEITA

Mwenyekiti wa Kijiji cha Ipandikilo kilichopo katika Halmshauri ya Wilaya ya Chato, Lazaro Kagundulilo (kulia), akizungumza na wanahabari pamoja na  wataalamu wa kilimo kutoka Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (Costech) na , Jukwaa la Bioteknojia na Uhandisi Jeni (OFAB), wilayani humo jana. Wataalamu hao wa kilimo wapo katika wilaya hiyo kwa ziara ya kutoa mafunzo ya kilimo chenye tija kwa maofisa ugani wa Mkoa wa Geita.


Maofisa ugani wakiangalia eneo ambalo patalimwa shamba dogo la mfano katika Kijiji cha Kibehe Kata ya Kigongo.
Mtaalamu wa masuala ya mizizi kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Ukiliguru jijini Mwanza, Dk. Jeremiah Simon (kulia),  akitoa maelezo kwa wanahabari wakati walipotembelea moja ya shamba la zao la mhogo lililokumbwa na ugonjwa wa batobato na michirizi ya kahawia wakati wa ziara hiyo katika Kijiji cha Ipandikilo.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Ipandikilo kilichopo katika Halmshauri ya Wilaya ya Chato, Lazaro Kagundulilo, akiwaonesha waandishi wa habari shina la mhogo lililoathiriwa na magonjwa.
Ofisa Program wa OFAB kutoka Shirika la AATF la nchini Kenya, Suleiman Okoth (kushoto), akiwaelekeza jambo Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Ipandikilo, Clara Fidelis (kulia) na Ofisa Ugani wa Wilaya ya Chato, Charles Ntaki.
Shamba la mhogo lililoathiriwa na magonjwa.
Wanahabari wakitoka shambani.
Wakulima wa Kijiji cha Ipandikilo wakimenya mihogo tayari kwa kuianikwa kwa ajili ya unga wa ugari. Kutoka kulia ni Veronica Zakaria, Joyce Joseph na Teloza Lugiyege.
Shamba la mhogo linaloonekana kustawi vizuri lakini tayari limeathiriwa na magonjwa ya batobato na mchirizi kahawia.
Mkulima Andrew Misano akitoa maelezo kwa wanahabari kuhusu changamoto mbalimbali za kilimo cha mhogo.
Mtaalamu wa masuala ya mizizi kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Ukiliguru jijini Mwanza, Dk. Jeremiah Simon (kushoto), akizungumza na wakulima wa kijiji cha Ipandikilo kuhusu mbegu bora za mhogo.
Mjumbe wa Kijiji cha Idoselo, Majeshi Mussa akiwaonesha waandishi wa habari mtama ulioathirika kwa kukosa mvua.

Na Dotto Mwaibale, Chato

MBEGU bora za zao la mhogo  zinazositahimili magonjwa ya Batobato na michirizi kahawia zinahitajika ili kuweza kunusuru kukumbwa na baa la njaa kwa wakulima wa zao hilo katika Wilaya ya Chato mkoani Geita baada ya mbegu walizolima msimu huu kushambuliwa na magonjwa.


Wananchi wa wilaya hiyo wanategemea zaidi zao la mhogo kama chakula chao kikuu pamoja na biashara lakini hivi sasa hali siyo shwari kutokana na mihogo waliyopanda kushambuliwa na magonjwa.

Akizungumza na wataalamu wa kilimo kutoka Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia na watafiti wa kilimo kutoka Jukwaa la Bioteknolojia Tanzania (OFAB), walio katika ziara ya kutoa mafunzo ya kilimo chenye tija wilayani humo leo, mkulima wa zao la mhogo katika Kijiji cha Ipandikilo, Andrew Misano alisema changamoto kubwa waliyonayo ni magonjwa yanayoshambulia zao hilo.

Misano alisema msimu wa mwaka huu umekuwa tofauti na misimu mingine kutokana na zao la mhongo kushambuliwa na magonjwa ya batobato na michilizi kahawia.

"Msimu huu nimelima ekari saba za mhogo lakini sitegemei kuvuna chochote kutokana na kushambuliwa na magonjwa hayo" alisema Misano.

Misano alisema kukosekana kwa  mbegu bora na inayostahimili magonjwa kumechangia wakulima kuwa na changamoto ya zao hilo katika maeneo mengi ya wilaya hiyo.

Kaimu Ofisa Kilimo na Umwagiliaji wa Wilaya ya Chato, Faidaya Isango alisema zao la mhogo katika wilaya hiyo limeshambuliwa na magonjwa kwa zaidi ya asilimia 60 katika Tarafa za Kechumba, Namilembe na Busilayombo ambapo ameeleza kuwa isipopatikana njia mbadala ipo hatari ya kuwepo uhaba mkubwa wa chakula.

Alisema changamoto nyingine kubwa iliyopo ni kwa wakulima kuendelea kung'ang'ania mazao ya mihogo iliyoshambuliwa na magonjwa badala ya kuing'oa kama wanavyoshauriwa na maofisa ugani ili isisambaze ugonjwa katika maeneo mengine.

Alisema kunasheria zimeandaliwa kwa ajili ya kuwabana wakulima wakaidi na zipo katika hatua ya kuanza kufanya kazi baada ya kupitishwa rasmi.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Ipandikilo Lazaro Kagundulilo alisema awali katika ekari tatu za mhogo kabla ugonjwa huo haujaanza walikuwa wakivuna magunia zaidi ya 25 lakini hivi sasa hawategemei kupata hata magunia matano jambo ambalo ni changamoto kubwa kwao.

Mtaalamu wa mizizi kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Ukiliguru Dk.Jeremiah Simoni alisema njia mbadala ya kuwasaidia wakulima hao ni kuanzisha mashamba darasa ambayo yataweza kutoa mbegu safi ambazo hazina magonjwa ya Batobato na michilizi kahawia kutokana na magonjwa hayo kutokuwa na dawa mbadala.

No comments: