Tangazo

September 19, 2017

SERIKALI ITAHAKIKISHA MIRADI YA UMEME, MBAGALA, KURASINI NA KIGAMBONI KUKAMILIKA KWA WAKATI

 Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani, (wakwanza kulia), Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania, (TANESCO), Mhandisi Dkt. Tito Mwinuka, (wakwanza kushoto), na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo anayeshughulikia Miradi, Mhandisi Khalid James, (watatu kushoto), wakimsikiliza Meneja Mradi wa TEDAP, Mhandisi Emmanuel Manirabona, (aliyenyoosha mkono), wakati Naibu Waziri na uongpozi wa TANESCO, ulipotembelea mradi wa TEDAP wa Gongolamboto jijini Dar es Salaam, Septemba 18, 2017. Mradi huo unahusu upanuzi na uendelezaji wa mradi wa kusafirisha umeme wa 132kv.

NA K-VIS BLOG/Khalfan Said

SERIKALI kupitia Shirika la Umeme Tanzania, (TANESCO), imeahidi kusimamia miradi ya umeme Kituo cha Tipper-Kigamboni,  Mbagala na Kurasini ili kuhakikisha inakamilika kwa haraka na kwa wakati na hatimaye wananchi wa maeneo hayo wanaondokana na adha ya kukatika kwa umeme mara kwa mara.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani, mwishoni mwa ziara yake ya kufuatilia uboreshaji wa vituo vya kupoza na kusambaza umeme pamoja na ujenzi wa kituo kipya cha kufua na kusambaza umeme huko Kimbiji  wilayani Kigamboni jijini Dar es Salaam Septemba 18, 2017.

Waziri pia amekagua ujenzi wa mradi wa maendeleo ya upanuzi na upatikanaji nishati (TEDAP), wa kusafirisha umeme wa 132kv ulioko Gongolamboto nje kidogo ya jiji.

“Wananchi wanataka umeme, hawahitaji kujua  nguzo za umeme zimepatikana wapi, au upembuzi yakinifu utakamilika lini, nimeagiza baada ya siku tano kuanzia leo (Septemba 18), fanyeni kazi usiku na mchana walau vituo viwili vya kupoza na kusambaza umeme viwe vimekamilika ili wananchi wa Mbagala na Kigamboni wapate umeme wa kutosha.” Alisema Dkt. Kalemani mbele ya Mbunge wa Kigamboni Dkt. Faustine Ndungulile, Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Mhe. Hashim Mgandila na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi, Dkt. Tito Mwinuka na viongizi wengine wa Tanesco.

Dkt. Kalemani alisema, miradi hiyo imechukua muda mrefu, na kwamba hakuna muda zaidi utakaoongezwa kuikamilisha.
Serikali kupitia TANESCO, inatekeleza miradi mitano ya kuongeza kiasi cha umeme kwenye maeneo ya Mbagala na maeeno kadhaa ya wilaya ya Temeke, Kurasini na Kigamboni ili kukabiliana na ongezeko la kasi la watu na shughuli za kiuchumi katika maeneo hayo.

Aidha Naibu Waziri aliipongeza TANESCO, kwa kutekeleza agizo lake la kuhakikisha wakazi 3,500 wa Kigamboni waliolipia ili kuunganishiwa umeme, wawe wameunganishiwa ifikapo Septemba 15, 2017 ikiwa ni pamoja na kupeleka nguzo za umeme zaidi ya 1,000 maagizo ambayo yametekelezwa.

Hata hivyo naibu Waziri alimueleza Mheshimiwa Mbunge wa Kigamboni na Mkuu wa Wilaya hiyo kuwa tiba mahsusi ya upungufu wa umeme kwenye wilaya hiyo ni kukamilika kwa ujenzi wa kituo kipya cha kupoza na kusambaza umeme cha Kimbiji.

“Tiba kubwa ya matatizo ya umeme kwa watu wa Kigamboni, na Mbagala ni hapa Kimbiji(kituo kipya), vile vituo vingine vitapunguza tu matatizo lakini naomba Mheshimiwa Mbunge, uwafikishie ujumbe wananchi kuwa Serikali ya awamu ya Tano inayo dhamira ya kweli ya kuhakikisha inawapatia umeme wa uhakika sio tu wananchi wa Kigamboni bali watanzania wote kwa ujumla.” Alifafanua Dkt. Kalemani.

Naibu Waziri ameshuhudia hatua mbalimbali za ukamilishaji wa miradi hiyo zikiwa zimefikiwa ambapo katika kituo maeneo yote aliyotembelea.

Kuhusu ujenzi wa kituo kipya cha Kimbiji, Dkt. Kalemani amemuagiza Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TANSCO, Mhandisi Dkt. Tito Mwinuka, kuwaleta mafundi wa TANESCO wealiotekeleza kwa muda mfupi ujenzi wa mradi wa kituo cha kupoza na ksuambaza umeme kule Mtwara ili waje kuongeza nguvu.
Mbunge wa Kigamboni Mhe. Dkt. Faustine Ndungulile, (kushoto), akizungumza mbele ya Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani ambaye alifuatana naye kwenye ziara hiyo.
Sakafu ya kufungia transfoma mpya ya umeme wa 15mva kituo cha Tipper-Kigamboni, ikijengwa Septemba 18, 2017
Mshine mpya kwenye kituo cha Mbagala
Kituo cha Kurasini ambacho nacho kitakuwa tayari baada ya siku tano.
Dkt. Kalemani, (katikati), Dkt. Ndungulile (wapili kushoto) na Dkt. Mwinuka, (wakwanza kushoto), wakiwa na Meneja wa Mradi wa TADEP, Mhandisi Emmanuel Manirabona, (kulia), baada ya kujionea moja ya mashine mpya ikiwa bado imefunikwa ili kuzuia vumbi kwenye kituo cha Kurasini.
Fundi akiwa kazini kwenye kituo cha Kurasini.
Naibu Waziri Dkt. Kalemani, na Mbunge wa Kigamboni Dkt. Ndungulile, wakiwa na furaha baada ya kutembelea kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Mbagala, ambacho ujenzi wake umekamilika
Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Mhe. Hashim Mgandila, akizungumza mwishoni mwa ziara ya Naibu Waziri, Dkt. Kalemani huko Kimbiji.
Naibu Waziri Dkt. Kalemani na Mhandisi Khalid James.
Msafara wa Naibu Waziri ukiwa kwenye eneo la mradi wa TEDAP. Gongolombaoto.
Mkandarasi anayejenga mradi wa TEDAP, Gongolamboto, akizunguzma.
Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, anayeshughulikia usambazaji umeme na huduma kwa wateja mama Joyce Ngahyoma, akielezea hatua zilizochukuliwa na TANESCO katika kuhakikisha wateja 3,500 wa TANESCO Kigamboni waliolipia gharama za kuunganishiwa umeme, wanapatiwa huduma hiyo ikiwa ni pamoja na kupelekwa kwa nguzo zaidi ya 1,000 kwenye eneo la Kigamboni. Anayemsikiliza ni Naibu Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani.
Kituo cha Mbagala
Dkt. Kalemani, (kushoto), akimsikiliza Meneja wa TANESCO Mkoa wa Temeke, Mhandisi Jahulula akielezea hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Tipper-Kigamboni.
Dkt. Kalemani, (wapili kushoto), akizungumza jambo na Mhandisi Dkt. Tito Mwinuka, walipowasili eneo la Kimbiji ambako kunatarajiwa kujengwa kituo kipya cha kupoza na kusambaza umeme kitakachohudumia wakazi wa Kigamboni, Kurasini na Mbagala. Wakwanza kushoto ni Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO nayeshughulikia Miradi, Mhandisi Khalid James.

No comments: