Tangazo

May 14, 2014

KUTOKA TASWA

KAMATI ya Utendaji ya Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) ilikutana Dar es Salaam juzi Jumatatu na kujadili masuala mbalimbali yahusiyo chama hicho.
 
A: Mjadala wa Michezo
Kikao kilikubaliana TASWA iendeshe mjadala kuhusiana na masuala mbalimbali ya kimichezo kila Jumatano ya kwanza ya  mwezi, ambapo wataalikwa  wataalamu mbalimbali kutoka vyama vya michezo, wanamichezo maarufu, wahariri wa habari za michezo na waandishi wa habari za michezo kujadili hoja husika.
 
Kutakuwa na wazungumzaji maalum kuhusu mada husika, ambapo wageni waalikwa watachangia kwa nia ya kuboresha kwa maslahi ya ustawi wa michezo hapa nchini.
 
Kwa kuanzia mjadala huo utafanyika Juni 4, mwaka huu katika ukumbi ambao utatangazwa hivi karibuni na mada itakuwa nafasi ya Tanzania katika Michezo ya Jumuiya ya Madola itakayofanyika Glasgow, Scotland kuanzia Julai 23 hadi Agosti 3 mwaka huu, ambapo Tanzania itashiriki katika michezo ya ngumi, riadha, kunyanyua vitu vizito, mpira wa meza, judo na kuogelea.
 
Pamoja na kuwaalika viongozi wa vyama mbalimbali vya michezo, pia utaratibu umeanza ili kuwaalika baadhi ya Watanzania waliopata medali katika mashindano hayo ili nao waweze kuzungumza na kuwahamasisha wanamichezo wa sasa wafanye vizuri.
 
B:TUZO ZA WANAMICHEZO BORA
 
Kamati ya Utendaji imepongeza juhudi zinazofanywa na Kamati ya Tuzo za Wanamichezo Bora inayoongozwa na Mkurugenzi wa Redio Times FM, Rehure Nyaulawa katika kuhakikisha tuzo hizo zinakuwa bora na za aina yake mwaka huu.
 
Tayari wadau kadhaa wameonesha nia ya kudhamini tuzo hizo, ambapo maelezo zaidi yatatolewa baada ya kikao cha Kamati ya Tuzo kufanyika Jumatatu wiki ijayo kujadili maendeleo kuhusiana na tuzo hizo.
 
C;UANZISHAJI WA SACCO’S
Kikao kiliteua wanachama sita wa TASWA, kuratibu na kuandaa Katiba ya Chama cha akiba na Mikopo (SACCO’S) kwa ajili ya wanachama wa TASWA na kusimamia uanzishwaji wake.
 
Kamati hiyo itaongozwa na Mhariri wa michezo wa gazeti HabariLeo, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Mikopo ya SACCO’S ya Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN), Mgaya Kingoba na Katibu wa kamati atakuwa Mhazini Mkuu wa TASWA, Shija Richard ambaye kitaaluma ni Mhasibu.
 
Wengine walioteuliwa ni Mhazini Msaidizi wa TASWA, Zena Chande, mwandishi wa habari wa TBC1, Angela Msangi, Mwandishi wa habari wa gazeti la Majira, Masau Bwire na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TASWA, Chacha Maginga. Kamati imepewa miezi mitatu kukamilisha mchakato huo kuanzia Juni mosi mwaka huu.
 
D; MAFUNZO
Kikao kilikubaliana kufanyike semina mbili kabla ya Agosti mwaka huu, ambapo bajeti ya suala hilo imeshapitishwa, hivyo sekreterieti ya TASWA imeagizwa kufanyia kazi suala hilo kwa kupanga Mkoa ambao itafanyika. Semina ya kwanza itafanyika Dar es Salaam na nyingine nje ya Mkoa wa Dar es Salaam. Kabla ya Jumanne wiki ijayo agizo hilo litakuwa limeshafanyiwa kazi.
 
Lengo la mafunzo hayo ni kuwekana sawa katika masuala mbalimbali ya kitaaluma na pia yale yahusiyo ripoti za michezo. Msisitizo ukiwa ni kuhakikisha wanachama wengi zaidi wa TASWA wanashiriki mafunzo yote hayo.
 
Kamati pia ilijadili kuhusiana na mafunzo ya waandishi chipukizi wanaotakiwa na Chama cha Kimataifa cha Waandishi wa Habari za Michezo (AIPS),  ambapo Makamu Mwenyekiti wa TASWA, Egbert Mkoko ameteuliwa kusimamia mchakato wa  kupata waandishi chipukizi ambao wasifu wao utatumwa AIPS ili waombewe kushiriki mafunzo hayo.
 
Hivyo kinachotakiwa waandishi wa habari za michezo ambao wana chini ya miaka minne katika fani na umri wao ni chini ya miaka 25, wana elimu kuanzia ngazi ya stashahada mpaka shahada watume wasifu wao binafsi na vyeti vya kitaaluma kwa Makamu Mwenyekiti TASWA kwa email: njali5@yahoo.com na taswatz@yahoo.com, ambapo mwisho ni Mei 30 mwaka huu.
 
E; MEDIA DAY
Hili pia lilijadiliwa kwa kirefu, ambapo mazungumzo na wadhamini bado yanaendelea na kesho Alhamisi kutakuwa na kikao kingine kati ya TASWA na wadhamini kuweka tarehe mpya ya tamasha hilo kwa mwaka huu.
 
Imetolewa na,
 Amir Mhando
Katibu Mkuu TASWA
14/05/2014

No comments: