Tangazo

August 14, 2015

BODI YA MIKOPO YAELEZEA MAFANIKIO MIKA 10 YA UHAI WAKE

Bw. Cosmas Mwaisobwa (katikati), Mkurugenzi Msaidizi (Habari, Elimu na Mawasiliano) wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) akiongea na wanahabari jijini Dar es Salaam leo (Ijumaa, Agosti 14, 2015). Wengine ni Bw. Omega Ngole, Meneja kutoka HESLB na Bi. Fatma Salum (kulia), Afisa Habari kutoka Idara ya Habari (MAELEZO).  Picha na HESLB.

--------


Na Mwandishi Wetu

Idadi ya wanafunzi wanaopata mikopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imeongezeka kutoka 42,729 mwaka 2005/200 wakati Bodi hiyo ilipoanza kazi hadi kufikia wanafunzi 98,000 kwa mwaka katika mwaka wa masomo 2014/2015.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo (Ijumaa, Agosti 14, 2015), Mkurugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa Bodi hiyo Bw. Cosmas Mwaisobwa amesema ongezeko hilo limetokana na Serikali kuongeza fedha za bajeti ya ukopeshaji wanafunzi inayotolewa kwa Bodi hiyo.  

Mafanikio
“Katika kipindi hicho cha miaka 10 ya uhai wa Bodi, bajeti ya fedha za mikopo zinazotolewa kwa wanafunzi imeongezeka kutoka Tshs 56.1 bilioni mwaka 2005/2006 hadi kufikia Tshs 345 katika mwaka wa fedha uliopita (2014/2015) na hivyo kuwezesha kuwakopesha wanafunzi hao,” amesema.

Bw. Mwaisobwa alikuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio na changamoto katika utekelezaji wajukumu ya Bodi hiyo katika kipindi cha miaka 10 ya uhai wake.

Akizungumzia urejeshaji wa mikopo iliyotolewa, Bw. Mwasobwa amesema HESLB imepata mafanikio makubwa kwa kuongeza kasi na kiasi cha fedha zinazokusanywa kama madeni kutoka kwa wanufaika.

“Katika kukusanya madeni nako tumepiga hatua kubwa kwani mwaka 2006/2007, tulikusanya Tshs 53.6 milioni tu lakini katika mwaka wa fedha uliopita pekee, tumekusanya Tshs 74.7 bilioni, hii ni hatua kubwa na inaiwezesha Serikali kukopesha wanafunzi wengi zaidi,” amesema.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Msaidizi huyo, ingawa HESLB ilianza kazi rasmi mwaka 2005, lakini sheria iliyoanzisha Bodi imeipa jukumu la kukusanya madeni ya mikopo ya wanafunzi iliyoanza kutolewa na serikali tangu mwaka 1994/1995 – kazi ambayo Bodi inaendelea nayo.

Mafanikio mengine aliyoyataja Bw. Mwaisobwa ni pamoja na kusogeza huduma karibu na wateja wa Bodi kwa kufungua ofisi nne za kanda katika mikoa ya Dodoma mwaka 2009; Mwanza (2014); Arusha (2015) na Zanzibar iliyofunguliwa mwaka 2011. Aidha, ameongeza kuwa idadi ya watumishi wa Bodi imeongezeka kutoka tisa mwaka 2005 hadi kufikia 135 hivi sasa.

Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, HESLB imeboresha utoaji wa huduma zake kwa kuanzisha utaratibu mpya wa kuomba mikopo kwa njia ya mtandao yaani ‘Online Loan Application and Management System (OLAMS)’.  Kupitia mfumo huu, waombaji wa mikopo wanaweza kuingia katika mtandao wa Bodi (www.olas.heslb.go.tz), kujaza fomu ya maombi na kuwasilisha fomu zao kwa njia ya mtandao kutoka popote walipo.

Changamoto
Pamoja na mafanikio hayo, kwa mujibu wa Bw. Mwaisobwa, Bodi ya Mikopo imekumbana na changamoto kadhaa katika kipindi cha miaka 10 iliyopita. Amezitaja changamoto hizo kuwa ni pamoja na kutokubalika ipasavyo kwa Sera ya Uchangiaji wa gharama za elimu ya juu na imani potofu kwamba mikopo inayotolewa na Bodi ni ruzuku na kwamba haipaswi kurejeshwa.

“Kuhusu hili la sera ya uchangiaji, kuna wananchi wanachangia huduma nyingine za kijamii, lakini kuchangia elimu hawataki...na kuhusu hili la imani potofu, kuna watu wenye uwezo wa kujigharamia elimu ya juu lakini wanaomba wakidhani ni ruzuku,” amefafanua Bw. Mwaisobwa na kuongeza kuwa changamoto nyingine kubwa ni baadhi ya wajiri kutotimiza wajibu wao wa kisheria wa kuwatambua na kuwasilisha taarifa za wanufaika wa mikopo kwa HESLB.

Hata hivyo, Bw. Mwaisobwa amesema Bodi itaendelea kujenga ushirikiano na kuwaelimisha waajiri na umma kwa ujumla kuhusu umuhimu wa kushirikiana na Bodi katika zoezi la kurejesha Mikopo na utekelezaji wa majukumu mengine.

Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) ni taasisi ya Serikali iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria Na. 9 ya mwaka 2004 na kuanza kazi rasmi mwezi Julai, 2005. Pamoja na majukumu mengine, ina wajibu wa kutoa mikopo kwa wanafunzi wahitaji; na kukusanya mikopo kutoka kwa wanufaika wa mikopo hiyo ili kuufanya mfuko wa mikopo ya elimu ya juu kuwa endelevu.

No comments: