Tangazo

October 29, 2012

Ongezeko la Joto Duniani ndicho chanzo cha Athari za mabadiliko ya tabianchi: Muyungi

Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Mazingira, Ofisi ya Makamu wa Rais, Bw. Richard Muyungi  (kulia), akifungua  warsha ya utambulishaji wa miradi pamoja na kujenga uelewa juu ya suala zima la kuhimili athari zitokanazo na mabadiliko ya tabia nchi, iliyofanyika mjini Bagamoyo leo. Kushoto ni Bw. Lars Christiansen Meneja kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Mazingira UNEP. (Picha na Evelyn Mkokoi) 

Sehemu ya washiriki wa warsha hiyo.

*************************
Evelyn Mkokoi wa OMR

Athari za mabadiliko ya tabianchi zitokanazo na kuongezeka kwa joto duniani zimezidi kudhihirika katika miaka ya hivi karibuni. 

Hayo yameelezwa leo na mkurugenzi msaidizi wa Idara ya mazingira Bw. Richard Muyungi, wakati wa ufunguzi wa warsha ya utambulishaji wa miradi pamoja na kujenga uelewa juu ya suala zima la kuhimili athari zitokanazo na mabadiliko ya tabia nchi, iliyofanyika mjini Bagamoyo.

Bw. Muyungi ameeleza kuwa, baadhi ya athari hizo ni pamoja na kuongezeka kwa kina cha bahari na matukio ya mara kwa mara ya ukame, vimbunga na mafuriko, mlipuko wa magonjwa kama vile malaria na kipindupindu.

Aliongeza kuwa, Ili kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliandaa Programu ya Kitaifa ya Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi mwaka 2007.

 “Kwa sasa nchi inamalizia maandalizi ya Mkakati wa Kitaifa kuhusu mabadiliko ya tabianchi ambao pamoja na mambo mengine, Mkakati umeainisha maeneo ya kipaumbele kitaifa katika kukabiliana na  mabadiliko ya tabianchi” Alisisita.

Aidha Bw. Muyungi alisema, Mradi wa kujenga uwezo wa kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi katika maeneo zalishi ya Pwani za Bagamoyo, Rufiji, Pangani na Zanzibar ni miongoni mwa maeneo ya kipaumbele ambayo yalibainishwa katika programu hiyo.

Mradi huo utahusisha Kuhifadhi mikoko, kukarabati na kuimarisha ukuta wa Bahari ulioharibika  katika mwambao wa pwani ya Pangani, kuhamisha visima vilivyoingiliwa na maji ya chumvi katika Wilaya ya Bagamoyo, uhifadhi wa mikoko katika mwambao wa Pwani ya Bahari ya Hindi katika wilaya ya  Rufiji.

Shughuli nyingine za mradi huo zitahusisha uhifadhi wa mikoko katika maeneo ya Tumbe na katika maeneo ya Ukele, Zanzibar, uhimarishaji wa ukuta wa Bahari maeneo ya Bwawani hoteli na kuhimarisha mikoko na kulinda maeneo ya ukanda wa Bahari Pemba, uhimarishaji wa ukuta wa Bahari maeneo ya Kisiwa Panza, Kukuza uelewa wa mabadiliko ya tabianchi na kutathmini madhara ya mabadiliko ya tabianchi katika jamii.pamoja na Kuuhisha integration suala la kuhimili mabadiliko ya tabianchi katika mipango ya maendeleo ya jamii.

Utekelezaji wa mradi huo umefadhiliwa na Mfuko wa mazingira wa dunia GEF kupitia Mfuko wanchi maskini zaidi Duniani. LDCF.

No comments: