Tangazo

September 8, 2014

OFISI YA TAIFA YA TAKWIMU YATOA TAARIFA YA MFUMUKO WA BEI NCHINI

Mkurugenzi wa Takwimu za Jamii na Sensa ya Watu na Makazi wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Bw. Ephraimu Kwesigabo akitoa taarifa ya mfumuko wa bei kwa mwezi Julai 2014 kwa waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam.
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Na. Aron Msigwa-MAELEZO.
Dar es salaam.
Ofisi ya Taifa ya Takwimu imeeleza kuwa  ongezeko dogo la mfumuko wa bei nchini kutoka asilimia 6.4 za mwezi June hadi asilimia 6.5 za mwezi Julai 2014 linatokana na kupanda kwa bei za baadhi ya bidhaa na huduma katika maeneo mbalimbali. 

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam Mkurugenzi wa Takwimu za Jamii na sensa ya Watu na Makazi Bw. Ephraim Kwesigabo amesema kuwa bidhaa zisizo za vyakula zikiwemo Bia, Sigara, mavazi kwa wanaume na yale ya watoto zimechangia ongezeko hilo.


Aidha, huduma na bidhaa nyingine zilizochangia ongezeko hilo ni gharama za udobi, kodi za pango, mazulia na mkaa wa kupikia   

Bw. Kwesigabo amefafanua kuwa hali ya mfumuko wa bei za bidhaa za vyakula na migahawa kwa mwezi Julai umepungua hadi 7.9 kutoka asilimia 8.5 kutoka asilimia 8.7 za mwezi Juni huku badiliko la fahirisi za bidhaa zisizo za vyakula likiongezeka hadi asilimia 4.9 kwa mwezi Julai 2014 kutoka asilimia 4.8 iliyokuwepo mwezi uliopita.

Kuhusu mfumuko wa bei unaopimwa kwa kipimo cha mwezi amesema kuwa umeongezeka kwa asilimia 0.1 ikilinganishwa na kupungua kwa asilimia 0.6 kama ilivyokuwa kwa mwezi Juni mwaka huu, huku fahirisi za bei za taifa zikiongezeka hadi kufikia 149.16 kutoka 148.98 za mwezi Juni 2014.

Kwa upande wa uwezo wa shilingi 100 ya Tanzania katika kununua bidhaa na huduma za jamii kutoka mwezi Septemba 2010 hadi Julai 2014 umefikia shilingi 67 na senti 04 kutoka shilingi 67 na senti 12 za mwezi Juni mwaka huu. 

“Kuongezeka  kwa bei ya baadhi ya bidhaa na huduma kwa mwezi uliopita kunamaanisha kwamba, uwezo wa fedha yetu katika kununua huduma na bidhaa hizo unaupungua hii inamaanisha mfumuko wa bei unapopanda thamani ya shilingi nayo inashuka” Amebainisha.

Kuhusu ulinganifu mfumuko wa bei wa Tanzania na baadhi ya nchi za Afrika Mashariki amesema kuwa una mwelekeo unaofanana na kueleza kuwa mfumuko wa bei nchini Kenya umeongezeka na kufikia asilimia 7.67 kwa mwezi Julai 2014 ikilinganishwa na asilimia 7.39 za mwezi Juni huku Uganda ikiwa na mfumuko wa bei wa asilimia 4.3 mwezi huu ikilinganishwa na  asilimia 5.0 za mwezi Juni.

No comments: