Na Anna Nkinda – Maelezo, New York
ZAIDI ya wasichana milioni 58 Duniani
wameolewa wakiwa na umri wa
chini ya miaka 18 kati ya hao milioni 15 wana umri wa
kati ya miaka 10 hadi 14 jambo linalowasababisha kupata maambukizi ya Ugonjwa
wa Ukimwi na kufanyiwa ukatili wa kijinsia.
Kwa upande wa Tanzania takwimu zinaonyesha
kuwa wasichana wanajihusisha mapema zaidi katika mapenzi ukilinganisha na
watoto wa kiume kwani asilimia 13 ya wasichana wanaanza kufanya mapenzi wakiwa
na umri wa chini ya miaka 15 wakati kwa upande wa wavulana ni asilimia saba.
Hayo yamesemwa leo na Mke wa Rais Dkt.
Jakaya Mrisho Kikwete Mama Salma Kikwete wakati akifungua mkutano uliojadili
elimu ya afya ya uzazi na jinsia kwa vijana ulioandaliwa na Waziri wa
Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo wa Ujerumani Gerd Mueller na kufanyika
katika ofisi za ubalozi wa nchi hiyo uliopo mjini New York nchini Marekani.
Mama Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa
Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) alisema kutokana na kitendo cha
wasichana kujihusisha na mapenzi wakiwa na umri mdogo wamekuwa wakikabiliwa na
tatizo la mimba za utotoni na hivyo wengi wao kushindwa kupata elimu.
“Nchini Tanzania kati ya msichana mmoja
hadi wanne wenye umri wa kati ya miaka 15 hadi 19 wana mimba au watoto , takwimu hizi ni
kubwa zaidi katika nchi zingine za kanda ya Afrika ya Mashariki na Kusini”.
Idadi hii inaonyesha wasichana wataendelea
kuwa kundi lililoathirika kwa kukosa haki zao za kupata afya, watakabiliana na
unyanyasaji na maisha yao yataisha mapema. Tukichukua hatua ya kuwasaidia sasa
tutaokoa wasichana wengi na
kuwasaidia kuwa na maisha mazuri hapo baadaye”, alisema Mama Kikwete.
Mwenyekiti huyo wa WAMA alisema vijana wa
Afrika wanatakiwa kupewa elimu ya maisha, afya ya uzazi na usawa wa jinsia
ambayo itaendana na mila na desturi zao ili waweze kuwa na uchaguzi mzuri wa
maisha yao kwani theluthi ya idadi ya watu wanaoishi nchi zilizopo Kusini mwa
jangwa la Sahara ni vijana wa kati ya miaka 20 na 24.
Mama Kikwete alisema, “Afrika ya baadaye
na ukubwa wa Dunia inategemea na jinsi tutakavyowaandaa vijana kujenga maisha
yao ya baadaye. Hii itawezekana kama tutawasaidia kuchagua njia nzuri kuhusu
afya yao na kuwaokoa kutoka katika tabia hatarishi”.
Kutimiza hili tunahitaji kuwa na elimu
bora ili mambo ya afya ya uzazi na stadi za maisha yapewe kipaumbele na
uangalizi mkubwa unatakiwa kwa watoto wa kike”.
Akiwakaribisha wadau wa elimu na afya
waliohudhuria mkutano huo Waziri wa Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo wa
Ujerumani Gerd Mueller alisema kwa zaidi ya miaka 20 Serikali yake imekuwa
ikifanya kazi ya kuhakikisha vifo vya kina mama wajawazito na watoto vinapungua
na upatikanaji wa huduma ya uzazi wa mpango inaimarika.
“Jambo la ziada linatakiwa kufanyika hasa
katika Bara la Afrika lenye matumaini tutaongeza ushirikiano tukilenga zaidi
katika elimu hasa elimu ya ufundi kwa wasichana na wavulana”.
Tunahitaji kufanya jambo la ziada kama
tunataka kufanikiwa katika afya na elimu kwa vijana hasa wasichana. Wasichana
wengi wenye umri wa chini ya miaka 18 katika nchi zinazoendelea wanapata mimba
zinazowaletea matatizo yanayopelekea vifo vyao”, alisema Mueller.
Alisema Serikali ya Ujerumani itatoa fedha
zingine Euro milioni 3 kwa ajili ya na kuandaa programu za pamoja ambazo
zitaongeza elimu ya afya ya ujinsia
na huduma za afya ya uzazi kwa vijana katika nchi za ukanda wa Afrika ya
Mashariki na Kusini.
Akichangia mada katika mkutano huo Mkurugenzi wa Kanda ya
Mashariki na Kusini mwa Afrika kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Kupamba na
Ukimwi (UNAIDS) Prof.
Sheila Tlou alisema vijana wanahitaji kupata elimu ya afya ya uzazi na jinsia
ili waweze kujikinga na ndoa za utotoni na Ugonjwa wa Ukimwi.
Takwimu zinaonyesha kwa kila saa moja kuna maambukizi mapya 50 ya
HIV kwa vijana hii ina maana kuwa kwa mwaka kuna maambukizi mapya 430000. Kwa
sasa kuna vijana milioni 2.6 wanaoishi na Virusi Vya Ukimwi (VVU).
Prof. Tlou alisema mwaka mmoja umepita
tangu Mawaziri wa Afya na
Elimu kutoka nchi 21 za Mashariki na Kusini mwa Afrika wakubaliane maazimio ya
kuongoza juhudi za kuandaa mazingira salama na wezeshi kwa makuzi ya vijana
katika nchi zao.
“Ni muhimu kuyafanyia kazi maazimio hayo ambayo yatawasaidia vijana kupata elimu kuhusiana na afya
ya uzazi na jinsia jambo ambalo litawasaidia kufahamu zaidi ugonjwa Ukimwi”,
alisema Prof. Tlou.
Mkutano huo ambao pia ulihudhuriwa na Mke
wa Rais wa Malawi Gertrude Mutharika ni moja ya maandalizi ya Mkutano wa 69 wa Umoja wa Mataifa (UN)
utaofanyika hivi karibuni mjini humo.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment