Tangazo

September 23, 2015

MJUMITA WASHINDA TUZO YA MAZINGIRA YA UN


Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo  wa Umoja wa Mataifa ( UNDP), Helen Clark (kushoto) akiwa na Mcheza  senema  maarufu na mwanaharakati wa Mazingira, Alec Baldwin (katikati)  na Mkewe, Hilaria Thomas wakati wa mkutano maalum na waandishi wa habari wa kutangaza washindi wa Tuzo ya Ikweta ambayo hutolewa na Umoja Mataifa kwa  NGO ambazo zinajihusisha na utunzaji wa  mazingira, ulinzi na uhifadhi wa misitu, matumizi bora na endelevu ya ardhi na mali asili na  kupiga vita umaskini. Tuzo ya mwaka huu wa 2015 ambayo ni  dola  za kimarekani 10, 000 kwa kila mshindi inakwenda kwa NGO 21 ambapo  NGO ya Tanzania ijulikanayo kama Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania ( MJUMITA) ni kati ya NGO sita kutoka Afrika,  Kusini  mwa Jangwa la Sahara zilizoshinda Tuzo hiyo. 
**************
MTANDAO wa Kijamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania (Mjumita) ni kati ya asasi   21 ambazo mwanzoni mwa wiki hii zimetangazwa kuwa washindi wa Tuzo ya Ikweta (Equator Prize) kwa mwaka 2015.


Tuzo hiyo hutolewa na Mfuko wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP) kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wanaofadhili tuzo hiyo. Kila shirika lisilo la kiserikali (NGO) iliyoshinda Tuzo hiyo inanyakua kitita cha Dola za Marekani 10,000.


Ushindi wa Mjumita pamoja na NGO nyingine 20 kutoka maeneo mengine duniani, ulitangazwa na Mkuu wa UNDP, Helen Clark katika mkutano wake na wawakilishi wa Muungano wa Waandishi wa Habari wa Umoja wa Mataifa.

Wawakilishi wa  NGO hizo   21 watapokeaTuzo zao Desemba mwaka huu, wakati wa Mkutano wa Kimataifa utakaojadili mabadiliko yaTabianchi ( COP21) utakofanyika Paris, Ufaransa.


Mjumita ni mtandao wenye wanachama katika vijiji 450 vilivyopo katika wilaya 23 za Tanzania na hujishughulisha na utunzaji wa misitu, kuwasaidia wanavijiji kupata hati za kimila za kumiliki ardhi, kutatua migogoro ya ardhi na kubuni miradi ya matumizi sahihi ya ardhi na rasilimali za misitu.


Taarifa iliyotumwa kwa gazeti hili ilieleza kuwa zaidi  ya watu 500,000 wamenufaika na huduma zinazotolewa na Mjumita.


Akizungumza wakati wa kuwatangaza washindi hao Clark aliyefuatana na Christiana Figueres anayeshughulikia masuala ya mabadiliko ya tabia nchi, alisema NGO hizo zinazojihusisha na masuala ya mazingira zimedhihirisha kuwa zina jambo la kuifundisha Jumuiya za Kimataifa.


Alisema zaidi ya washiriki 100 waliingia katika shindano hilo lakini  21 ndio walioibuka kidedea.


Clark alisema tuzo hiyo inatolewa wakati ambao viongozi wakuu wa mataifa mbalimbali wanakutana jijini New York kuzungumzia ajenda 17 za maendeleo endelevu ikiwamo namba 13 inayohusus mabadiliko ya tabia nchi.

No comments: