Tangazo

March 10, 2016

TRA YAKUSANYA TRILIONI 8.569 KWA KIPINDI CHA JULAI 2015 – FEBRUARI 2016

Kaimu Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Alphayo Kidata (wa pili kulia), akizungumza na waandihi wa habari jijini Dar es Salaam jana, kuhusu mwenendo wa ukusanyaji mapato, matumizi ya mashine za EFD, kusitishwa kwa bei elekezi  na usajili wa vyombo vya moto. Kushoto ni Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi, Richard Kayombo, Kaimu Kamishna wa Forodha, Qamdiyay Akonaay (wa pili kushoto), na Kaimu Kamishna wa Kodi za Ndani, Salum Yusuf. PICHA: JOHN BADI
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Dar es Salaam

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) yatoa ripoti ya mapato yaliyokusanywa kuanzia Julai 2015 hadi Februari mwaka huu ambapo yamefikia Sh8.569 trilioni ikiwa ni asilimia 99 ya malengo.

Kaimu Kamishna Mkuu wa TRA, Alphayo Kidata aliwaambia wanahabari jana Machi 09.2016, kuwa kwa kipindi hicho walipanga kukusanya Sh8.685 trilioni lakini hawakufikia lengo kutokana na kushuka na kupanda kwa kodi na kuahidi kuwa hadi ifikapo Juni, watakuwa wamefikia asilimia 100 ya malengo kwa mwaka wa fedha 2015/16.

Katika mkutano huo uliolenga kutoa mwenendo wa ukusanyaji mapato, matumizi ya mashine za kielektroniki za utoaji risiti (EFD), kusitisha bei elekezi katika ukadiriaji wa kodi na usajili wa vyombo vya moto, Kidata alisema malengo kwa mwaka huu wa fedha ni kukusanya Sh12.3 trilioni katika bajeti ya Sh22.4 trilioni iliyopangwa mwaka 2015/16.

Ripoti hiyo inaonyesha kuwa sehemu kubwa ya mapato hayo ilichangiwa na makusanyo ya kuanzia Desemba 2015 ambayo TRA ilikusanya Sh1.4 trilioni na kufuatiwa na Januari (Sh1.07 trilioni) na mwezi uliopita Sh1.04 trilioni.

Kidata alisema kuongezeka kwa mapato hayo kunatokana na kudhibiti mianya ya ukwepaji kodi na kuweka mazingira rafiki kwa mlipakodi, kurekebishwa kwa misamaha ya kodi iliyokuwa inachangia upotevu wa mapato, kuongezeka kwa watumiaji wa EFD na kudhibiti eneo la forodha.

Kaimu Kamishna wa Kodi za Ndani wa TRA, Salum Yusuf alisema mamlaka hiyo inaendelea kugawa mashine za EFD bure kwa wafanyabiashara wadogo ambao uwezo wa kununua mashine hizo unaweza kuathiri mitaji yao ya biashara na kwamba tayari wameshakamilisha ununuzi wa mashine za uniti 5,700.

Kidata alisema TRA, imefanya ukaguzi na kubaini kuwepo kwa magari ambayo yaliingizwa nchini na kusajiliwa bila kufuata taratibu za forodha hivyo kuyafanya yamilikiwe bila kulipiwa kodi stahiki. Sehemu kubwa ya magari hayo, alisema yaliingizwa kutokana na matumizi mabaya ya misamaha ya kodi.

Katika hatua nyingine, Mamlaka hiyo imefuta bei elekezi katika mchakato wa uthaminishaji wa bidhaa bandarini kwa sababu ni kinyume cha sheria ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na kwamba TRA itaendesha shughuli za forodha kulingana na sheria husika.

Tumeona bei elekezi haisaidii kwa sababu uingizaji wa bidhaa unatawaliwa na sheria ya Afrika Mashariki ambayo Tanzania ni wanachama, hivyo Mamlaka itadhibiti ukaguzi na uthaminishaji halisi ili kila mfanyabiashara alipe ushuru na kodi kulingana na thamani ya bidhaa husika,” alisema Kidata.  

No comments: