Tangazo

November 15, 2011

Tanzania Mwenyeji wa mkutano wa upimaji ardhi na ramani

Prof. Anna Tibaijuka
Na Anna Nkinda – Maelezo

Tanzania inatarajiwa kuwa mwenyeji wa mkutano wa 45 wa upimaji ardhi na ramani ambao utawahusisha  Makatibu Wakuu wanaofanya kazi katika wizara zinazoshughulikia  sekta ya ardhi  kutoka nchi 18 Barani  Afrika.

Mkutano huo wa siku mbili  ambao umeandaliwa  na Wizara ya Ardhi, Nyumba  na Maendeleo ya Makazi kwa kushirikiana na  kituo cha Regional Center for Mapping of Resources for Development unatarajia kuanza tarehe 17-18 mwezi huu katika hoteli ya Double Tree jijini Dar es Salaam.

Washiriki wa mkutano huo ambao utafunguliwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba  na Maendeleo ya Makazi Prof. Anna Tibaijuka ni Nchi wanachama wa kituo hicho ambazo ni Tanzania, Botswana, Burundi, Comoros, Ethiopia, Kenya, Lesotho, Malawi, Mauritius, Namibia, Rwanda, Seychelles, Somalia, Afrika ya Kusini, Sudan, Swaziland, Uganda na Zambia.

Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Wakurugenzi wa Upimaji na Ramani ambaye pia ni Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani kutoka wizara ya Ardhi Dk. Selassie  Mayunga amesema kuwa hivi sasa kamati hiyo inaendelea na mkutano wake wa siku tatu ambao unajadili masuala mbalimbalikuhusiana na  ardhi kwa nchi wanachama na baada ya hapo utafuatia mkutano wa Makatibu wakuu.

Akieleze kuhusu kituo cha Regional Center for Mapping of Resources for Development Dk. Mayunga anasema kuwa kinaendeshwa kwa michango ya nchi wanachama. Kila nchi inachangia kutokana na uchumi wake ambapo kwa mwaka wa fedha 2011/12 Tanzania imechangia dola za Kimarekani 65,000/= ambazo zitatumika kuendesha kituo na kutoa mafunzo kwa nchi wanachama.

“Tanzania kama mwanachama inafaidika na kituo hiki kwani inatuma wataalamu wake kwenda kujifunza mambo mbalimbali ya upimaji na ramani, utunzaji wa mazingira, usalama wa vyakula  na fedha zinazogharamia mafunzo haya ni mchango tunaotoa kila mwaka”, alisema Dk. Mayunga.

Alimalizia kwa kusema kuwa ni heshima kubwa kwa Tanzania kuandaa mkutano mkubwa kama huo na watatupia  fursa hiyo kujitangaza jinsi walivyofanikiwa katika suala la upimaji ardhi na wanaamini kuwa maadhimio yatakayopatikana yatasaidia kuimarisha shughuli za upimaji ardhi, utunzaji wa mazingira na kupatikana kwa mafunzo ya mara kwa mara kwa nchi wanachama.

Kwa upande wake Afisa Mahusiano wa kituo hicho Byron Anangwe alisema kuwa kazi kubwa wanayoifanya ni kuzishauri Serikali za nchi wanachama kuhusiana na mambo ya mipaka, uongozi wa ardhi, utunzaji wa mazingira, usalama wa vyakula  na  wanafanya kazi zao kwa kutumia  satelite.

Alisema kuwa wameshatoa mafunzo ya kuwajengea uwezo zaidi ya wafanyakazi 1000 kutoka katika nchi wanachama  katika upimaji wa ardhi, kutunza mazingira na technolojia ya jinsi ya kutumia software  zisizo na malipo kama google katika masuala ya upimaji na ramani.

Kwa mujibu wa kanuni na Sheria zilizowekwa na waanzilishi wa kituo cha Regional Center for Mapping of Recourses for Development mkutano huo hufanyika kila mwaka  na kwa mara ya mwisho ulifanyika mwaka jana huko Capetown Nchini Afrika ya Kusini.

Mawaziri wa wizara zinazoshughulikia sekta ya Ardhi wanakutana kila baada ya miaka miwili huku lengo kuu la mikutano hiyo likiwa ni  kuzisaidia nchi wanachama katika masuala ya upimaji na ramani.

Tanzania ni moja ya nchi waanzilishi wa umoja huo ambao ulianzishwa mwaka mwaka 1975  huko Nairobi nchini  Kenya huku waanzilishi wengine  wakiwa ni Kenya, Uganda, Somalia na Malawi.

No comments: