Tangazo

January 16, 2014

‘Warioba chanzo cha Serikali tatu’

Adai alipinga Muungano wa Serikali mbili tangu enzi za Nyerere, alikuwa miongoni mwa waliounda kundi la G55 .

Moshi. 

Mwanasiasa mkongwe nchini, Peter Kisumo (pichani),  amesema haafiki mapendekezo yaliyomo katika rasimu ya pili ya Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano yanayopendekeza muundo wa Serikali tatu.

Kisumo alisema hashangai kuona jinsi Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba alivyojitahidi kujenga hoja ya Serikali tatu na kusema, tangu zamani anamfahamu alikuwa kundi la G55.

Agosti 1993, wabunge 55 waliopewa jina la G55 wakiongozwa na Mbunge wa Lupa, Njelu Kasaka waliwasilisha bungeni hoja ya kutaka kuundwa kwa Serikali ya Tanganyika ndani ya Muungano.

“Na hili si la kificho hata kidogo kwamba yeye (Warioba) alikuwa kwenye kundi lile la G55 na wakati ule hakuonekana sana kwa sababu alikuwa akimuogopa Nyerere (Baba wa Taifa),”alisema Kisumo.

Kisumo amesema, yeye anaamini muundo wa Serikali mbili kama ulivyo sasa ndiyo mwafaka katika kulinda Muungano, na kwamba kama kuna kasoro zilizoainishwa na tume basi zitazamwe upya.

“Bila shaka gharama za kuendesha Serikali ya Muungano itabebwa na Tanganyika...Tunabebeshwa mzigo bure hao wanaotaka uhuru kamili (Zanzibar) ndiyo wabebeshwe gharama za Serikali ya tatu”.

Kisumo alisema busara ya kawaida ilimtaka Jaji Warioba pia aeleze faida za Serikali mbili ili Watanzania waweze kupima lakini hilo akalikwepa kwa makusudi ili kuhalalisha hoja yake.

“Muundo wa Serikali tatu utaleta mgogoro wa kikatiba, aliposema Watanzania wengi wanataka Serikali yao (Tanganyika) mbona idadi ya waliowafikia ni ndogo sana, hakuyasema kabisa?”alihoji Kisumo

Kisumo alisema kama kweli kuna Watanzania wengi wanataka kuundwa kwa Serikali ya Tanganyika basi hilo litajidhihirisha kwenye kura ya maoni huku akisisitiza kwamba haamini iwapo kuna watu wanaotaka Tanganyika.
Chanzo: Mwananchi Januari 15/2014

No comments: