Tangazo

October 19, 2012

Malindi kujinasua mkiani Ligi Kuu ya Grand Malt?

Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
 LIGI Kuu ya Grand Malt ya Zanzibar inatarajiwa kuendelea tena leo kwa mchezo mmoja, huku swali kubwa likiwa ni kama Malindi itaweza kujinasua kutoka mkiani pale itakapoivaa Jamhuri mchezo unaotarajiwa kufanyika Uwanja wa Amaan, Zanzibar.

Iwapo itafanikiwa kushinda mchezo huo, Malindi inayoshika mkia ikiwa na pointi tatu kwa michezo saba iliyocheza, itapanda kwa nafasi moja zaidi na kuishusha Falcan yenye pointi tano.
Jamhuri hata ikifungwa itabaki katika nafasi ya saba, lakini ikishinda nayo itapanda kwa nafasi moja na kuishusha Duma yenye point nane.

Mchezo huo ni muhimu zaidi kwa Malindi inayotaka kurejesha heshima yake, huku ikiwategemea washambuliaji wake wakali Amour Suleiman na Mussa Omar katika kuzifumania nyavu, huku Jamhuri wakimpa majukumu Mfaume Shaaban.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea tena kesho kwa michezo miwili wakati Zimamoto watakapoumana na Mafunzo katika Uwanja wa Amaan, Unguja huku Duma ikikwaana na Bandari ndani ya Uwanja wa Gombani, Pemba.
Mafunzo ndio wanaoongoza ligi hiyo wakiwa na pointi 14 wakifuatiwa na Chipukizi iliyo na pointi 13 na Bandari wanakamata nafasi ya tatu wakiwa na pointi kama hizo.
Bado mshambuliaji wa Chipukizi, Faki Mwalim anaongoza kwa kufunga mabao, kwani mpaka sasa ana mabao matano akifuatiwa na Ali Mnyovela wa Mtende na Jaku Jome Jaku wa Mafunzo wenye mabao manne kila mmoja.

No comments: