Tangazo

September 12, 2014

Uimarishaji zao la Karafuu faraja kwa wananchi Zanzibar

Mkurugenzi Mwendeshaji ZSTC, Mwanahiji Almas Ali 
 .Mikopo nafuu kwa wakulima yarahisisha shughuli za uchumaji


. Serikali inatoa bure miche 1,000,000 Unguja na Pemba

.Azma ya Serikali ni kuendelea kuwapatia wakulima bei nzuri

Zanzibar
ZANZIBAR ni visiwa vinavyosifika kwa uzalishaji wa karafuu bora duniani. Katika miaka 30 ya nyuma pia ilisifika kwa uzalishaji karafuu nyingi, zaidi ya tani 6,000 zilikuwa zikizalishwa kwa mwaka.

Wazee wetu wakati huo walikuwa wakizijali, wakizithamini na wakizipenda sana karafuu ukilinganisha na kizazi cha sasa. Walihakikisha karafuu zao wakiuza vituoni tena zikiwa safi, zimekauka vizuri na kupata daraja la kwanza.

Zao la karafuu linaongoza katika kuingiza kipato kwa wananchi na Taifa miongoni mwa mazao yanayozalishwa Zanzibar na linaendelea kuwa chanzo muhimu cha fedha za kigeni kwa Taifa baada ya sekta ya utalii.

Kwa sababu hiyo, ndio zao hilo linaendelea kuwa chini ya udhibiti na uangalizi makini wa Serikali kupitia Shirika la Biashara la Taifa Zanzibar (ZSTC), chini ya sheria namba 39 ya mwaka 1968 ili zao hili liendelee kuwa na tija zaidi kwa wakulima, wananchi na Taifa kwa jumla.

Kutokana na umuhimu huo wa zao la karafuu kwa maendeleo ya kiuchumi na ustawi wa wananchi, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imechukua jitihada zote kuliimarisha zao hili ili kuongeza uzalishaji, tija na ubora katika soko la dunia.

JITIHADA ZA ZSTC
- Katika kuongeza kiwango cha uzalishaji, usafirishaji na ubora wa karafuu Serikali imeongeza bei ya karafuu na mkulima anapata asilimia 80 ya bei ili kumuwezesha mkulima kumudu gharama za uzalishaji kama vile kupanda miche na kuishughulikia hadi izae na kusafisha mashamba.

- Kupitia Wizara ya Kilimo na Mali Asili Zanzibar na Shirika la ZSTC, Serikali inazalisha miche 1,000,000 na kutolewa bure kwa Wakulima Unguja na Pemba kila mwaka ambapo wakulima wanahimizwa kuipanda na kuishughulikia hadi izae.

- ZSTC inatoa mikopo nafuu kwa wakulima katika kurahisisha shughuli za uchumaji. Mikopo hiyo ni kwa ajili ya maandalizi ya awali ya uchumaji kama vile kujenga kambi, kununua majamvi na kuwalipa vibarua.

- ZSTC imeviimarisha vituo vya zamani na kujenga vituo vipya vya manunuzi karibu na wakulima ili kurahisisha shughuli za usafirishaji wa karafuu. Katika vituo hivyo kuna huduma zote muhimu kama vile umeme, vyoo, vikalio, ulinzi na wakulima wanapata huduma ya tende na kahawa katika vituo hivyo.

- Sambasamba na uimarishaji huo wa vituo vya manunuzi, ZSTC imeweka mizani mpya pamoja na kuimarisha huduma nyengine katika vituo vya manunuzi ambapo vituo hivyo vinalingana na hadhi na thamani ya karafuu.

- Serikali inaendelea na mpango wa kuifanya karafuu ya Zanzibar ijuulikane dunia nzima kutokana na sifa zake za kipekee za ubora kupitia mradi wa Tasnia ya Mali Bunifu (BRANDING). Mradi huu utaongera thamani na ubora wa karafuu ya Zanzibar duniani. 
 MAMBO YA KUFANYA
Wakulima na wadau wa zao la karafuu ni vyema wakaunga mkono jitihada hizi za Serikali kwa kuhakikisha sifa nzuri za ubora wa karafuu  za Zanzibar zinaendelea kwa kufanya yafuatayo:

- Tuhakikishe karafuu zinauzwa katika vituo vya ZSTC na karafuu hizo tuhakikishe zinakuwa safi na zisiwe na zaidi ya asilimia 2% ya takataka.

- Tuhakikishe karafuu zinazopelekwa kuuzwa katika vituo vya ZSTC zinakauka ipasavyo na zisiwe na zaidi ya asilimia 14% ya unyevu.

- Tutumie jua kwa kuanikia karafuu na si kuzikaanga au kutumia mbinu nyengine kuzikausha.

- Tuhakikishe karafuu zinazopelekwa kuuzwa katika vituo vya ZSTC hazichanganywi na unga wa makonyo, matende, mpeta na vitu vyengine visivyohitajika.

- Tuhakikishe karafuu zinachumwa zikiwa zimepevuka vizuri.

- Tuhakikishe karafuu tunazianika katika sehemu nzuri na safi kwa kutumia majamvi.

- Tuhakikishe hakuna magendo ya miche ya mikarafuu wala karafuu zenyewe ili kulinda pato la Taifa linalotokana na zao la karafuu.

- Kama ilivyo kawaida ya muda wa kazi, Vituo vinafunguliwa saa 1:30 asubuhi hadi 9:30 jioni, tunatakiwa tufuate utaratibu wa mda wa Vituoni.

- Tuhakikishe kila Mdau wa zao la karafuu anatimiza wajibu wake ipasavyo ili ubora wa karafuu za Zanzibar usipotee kirahisi.

AZMA YA SERIKALI
Sera ya serikali ya zao la karafuu ni kumnufaisha mkulima zaidi hivyo Serikali  itaendelea na azma yake ya kutekeleza uamuzi wake wa kuwapatia wakulima bei ya karafuu ya asilimia 80 ya bei ya soko la nje.

Hiyo ilikuwa ni kauli ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, wakati alipokuwa akizindua rasmi msimu wa ununuzi wa karafuu wa mwaka 2014/2015 uliofanyika Mkoani, Kusini Pemba.

Alibainisha kuwa huo ni uamuzi wa kisera na kwamba Serikali haitarudi nyuma kwa kuwa lengo lake ni kuhakikisha kuwa zao la karafuu linaendelea kuwa zao la biashara kwa Zanzibar.

Alieleza kuwapatia wakulima bei hiyo ni miongoni mwa hatua nyingi zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Saba kuhakikisha karafuu za Zanzibar zinaendelea kuwa na ubora wake na kubakia kuwa kitambulisho cha Zanzibar.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mwendeshaji wa ZSTC Bi Mwanahija Almas Ali bei ya asilimia 80 imekuza usatawi wa wananchi na imetoa ari kwa wakulima kupanda mikarafuu na pia imepunguza usafirishaji wa karafuu isivyo halali na imeongeza pato la Taifa.

Dk. Shein alizitaja hatua nyingine kuwa ni pamoja na kuimarisha huduma za ununuzi wa karafuu, kujenga barabara kwenye maeneo yenye karafuu nyingi, kutoa miche ya mikarafuu kwa wakulima, kutafuta masoko ya nje na kuwatia mikopo wakulima.

Hatua nyingine alieleza Dk.Shein, ni kufanya uamuzi wa kulifanyia marekebisho makubwa shirika la ZSTC ili liweze kutekeleza majukumu yake kulingana na mazingira ya sasa na matokeo yake mafanikio makubwa yameonekana tangu mabadiliko hayo kufanyika.

Hata hivyo Dk Shein alieleza kutoridhidhwa kwake na hatua ya baadhi ya wakulima kutorejesha mikopo kwa Shirika hivyo alitoa wito kwa wakulima hao kurejesha mikopo hiyo kwani Serikali haingependa kuwapeleka wananchi hao katika vyombo vya sheria.

Dk. Shein alihimiza jitihada zaidi kwa wakulima wa karafuu pamoja na wananchi kwa jumla kutilia mkazo ulinzi katika mashamba ya karafuu ili kudhibiti wizi wa zao hilo na kukemea vitendo vya baadhi ya wezi wa karafuu hukata matawi ya mikarafuu wakati wakifanya vitendo hivyo viovu.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi alitumia fursa hiyo kulipongeza shirika la ZSTC kwa kutekeleza mabadiliko makubwa ya muundo na mfumo wa utendaji hadi kulifanya shirika hilo sio tu kujiendesha kibiashara, lakini pia kupata ufanisi mkubwa katika shughuli zake.

Kwa wa Waziri wa Biashara, viwanda na Masoko, Ahmed Mazrui, alirejea wito wa Serikali kuwataka wakulima wa karafuu kuzingatia utunzaji mzuri wa karafuu tangu wakati wa kuchuma hadi zinapopelekwa katika vituo vya ununuzi.

Aliwataka wakulima kuzianika karafuu katika majamvi ili kulinda ubora wake na kuwahakikishia kuwa serikali kupitia Shirika la ZSTC imejiandaa vya kutosha kwa vifaa na masuala mengine muhimu kwa ajili kufanikisha kazi hiyo.  
Waziri wa Biashara Nassor Ahmed Mazurui (wa pili kushoto).
HISTORIA YA KILIMO CHA KARAFUU

Historia ya kilimo cha karafuu na hali ya upandaji wa mikarafuu visiwani Zanzibar 
Karafuu ni zao linalotokana na mkarafuu, ingawa karafuu hazimo katika kundi la vyakula wala vinywaji, lakini ni kiungo muhimu sana. Karafuu zina matumizi kadha, wakati fulani zinatumika kwenye utengenezaji wa sigara, upishi, utengenezaji wa aina fulani ya dawa ya meno na pia mafuta yake hutumika kwa kuchua misuli.

Kutokana na kitabu cha historia, mikarafuu ilianza kupandwa kwenye visiwa vya Shelisheli, Mauritius na sehemu nyinginezo. Miche ya mkarafuu ililetwa Zanzibar kutoka Mauritius mwaka 1818, miti hii imestawi zaidi Visiwani Unguja na Pemba ambavyo vinatoa asilimia 80 ya karafuu zinazohitajika duniani. Uchumi wa visiwa vya Zanzibar unategemea sana zao la karafuu.

Historia ya upandaji wa karafuu visiwani Zanzibar inatuonyesha ilianza zamani sana. Miche ya mikarafuu kuja kwake hapa ilitokana na visiwa vya Indonesia, mashariki ya mbali, ilifika huko Madagasca na Shelisheli katika karne ya 19 na ndiyo ikakuja Zanzibar na kupandwa wakati Wafalme wa Oman walipotawala.

Kimbunga kiliwahi kutokea na na kiling'oa mikarafuu mingi, kwa hivyo kukawa na juhudi mpya ya Wafalme wa wakati ule kupanda mikarafuu mipya. Ilikuwa si  kitu hiari, bali ilikuwa  jambo la lazima, watu wapande mikarafuu kwa sababu kitu hicho kinasaidia uchumi.
Kabla ya mapinduzi, mashamba ya mikarafuu yalikuwa ni ya watu binafsi, lakini baada ya mapinduzi, serikali ilitaifisha ardhi na kuigawa kwa wananchi. Kila mwananchi alipata eka tatu za kumuwezesha kulima, kupata chakula chake na kupata mahitaji yake ili ajiendeleze na familia yake.

Hiyo imeendelea mpaka leo, kwa hiyo sasa suala la karafuu linamilikiwa na wananchi wenyewe. Idadi kubwa ya mashamba yalikuwepo ni ya wananchi wenyewe. Ingawa kuna maeneo ya serikali, maeneo yanayomilikiwa na serikali ambayo yana karafuu na serikali inawakodisha watu ambao wanataka kukodi, kuchuma na kuuza, mashamba hayo yapo Zanzibar na Pemba.

Utaratibu wa uatikaji, ugawaji na upandaji wa miche ya mikarafuu bado unashughulikiwa na Wizara ya Kilimo ambayo  ndiyo iliyopewa jukumu hilo kwa kushirikiana na Shirika la Taifa la Biashara ZSTC, ZSTC waniwezesha Wizara ya kilimo kwa kiipa fedha.

Serikali kupitia ZSTC inachangia maendeleo ya zao la karafuu kwa kiwango kikubwa. Inawalipa vibarua wanaoshughulikia kuendeleza upandaji wa mikarafuu mipya katika sehemu mbalimbali ambazo mikarafuu imekufa, ZSTC inanunua zana za kutengeneza miche na kupanda miche mpaka kuisambaza kwa wananchi.

Kwa muntadha huo, ZSTC inajukumu kubwa la kuendeleza zao la karafuu na kulifanya likubalike kimataifa na kuwainua wakulima visiwani humo huku mtazamo wa sasa wa hali ya kibiashara ya nje ni kutafuta mazao zaidi ya karafuu pamoja na kuzalisha bidhaa zitokanazo na zao hilo la karafuu (Packages).

ZSTC kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo inaendelea kutekeleza mkakati wa kuimarisha zao la karafuu kwa kuotesha miche mingi hadi kufikia milioni moja kwa mwaka na kuwagaia wakulima.

Awali ZSTC ilikuwa ikitumia si zaidi ya shilingi bilioni tano kununulia karafuu, lakini, sasa linatumia zaidi ya bilioni 60 hali ambayo inathibitisha maendeleo makubwa yaliofikiwa hadi sasa na shirika hilo la umma.

Malengo ya baadae ya ZSTC ni kuendelea kuliimarisha zao la karafuu na kuhakikisha linachukuwa nafasi ya kwanza katika kuchangia pato la taifa na fedha za kigeni ambapo kwa sasa inashikiliwa na sekta ya utalii.


'KARAFUU NI UHAI WA UCHUMI NA USTAWI WA ZANZIBAR'

No comments: