Tangazo

September 17, 2012

JIHADHALI NA UTAPELI WA DAWA ZA MIFUGO ZA GUSTAVIC ANIMAL VACCINE

MTU mmoja raia wa Ujerumani, amewaliza Watanzania wengi baada ya kufanikiwa kuiba kwa njia za kitapeli mamilioni ya fedha.

Raia huyo ambaye amekuwa akibadilisha majina, kwa zaidi ya miezi miwili sasa, amejichimbia katika hoteli kubwa za kitalii akijifanya kuwa wakala wa dawa za mifugo na wanyama kwa kushirikiana na watu wengine watatu raia wa Tanzania.

Habari za kuaminika zilizothibitishwa na askari polisi jijini Dar es Salaam, zimesema mjerumani huyo anayekisiwa kuwa na umri kati ya miaka 65 na 70, amekuwa akitumia jina la kampuni moja kubwa ya dawa za mifugo (jina linahifadhiwa) ya hapa nchini kufanikiwa utapeli huo.

Mmoja wa watu waliotapeliwa, Martin Peter, alisema wiki iliyopita, mjerumani huyo pamoja na Watanzania watatu, walifanikiwa kumtapeli jumla ya shs milioni 25, kwa ahadi ya kumpa zabuni ya kuuza dawa za mifugo katika mkoa wa Katavi.

Akisimulia kwa undani alivyotapeliwa, Mariselina alisema: “Jumanne wiki iliyopita, nilipigiwa simu na mtu aliyejitambulisha kwa jina la Martin ambaye alisema tulisoma naye sekondari zaidi ya miaka 10 iliyopita.

“Ingawa sauti sikuwa naikumbuka, lakini baada ya kujieleza, nilikumbuka kwamba ni kweli nilisoma na mvulana huyo na alikuwa rafiki yangu.”

Mariselina alisema kuwa ‘rafiki’ yake huyo, alimwambia kuwa kwa sasa yuko mkoani Katavi katika shirika la hifadhi ya taifa, na kwamba alikuwa akihitaji amsaidie kupata dawa za wanyama kwa kuwa kulikuwa na mlipuko wa ugonjwa katika hifadhi hizo.

“Aliniambia kuwa anahitaji nimsaidie kwenda katika kampuni ya (anaitaja) na kuonana na (anamtaja) ambaye anasema kuwa huwauzia dawa hizo kila wakati.

“Alisema safari hii hataki kununua kwake, kwa vile amekuwa hampi cha juu (bakshishi), na kwa sasa ameona anitafute mimi ambaye niliwahi kumsaidia tukiwa shuleni ili nami nipate faida kidogo,” alisema.

Mariselina aliendelea kudai kuwa, Martin alimpa namba ya mtu huyo wa kampuni ya dawa, na kwamba akiisha inunua, aende hadi katika hoteli ya kitalii ya (anaitaja) ambako atamkuta mkuu wake wa kazi, ambaye ni raia wa ujerumani ambaye atanunua dawa hizo.

Mama huyo amedai, awali aliingiwa na hofu, lakini akapata nguvu baada ya kupiga simu na mtu wa kampuni ya dawa aliyekubali kumuuzia dawa.

“Martin pia alinipa namba za huyo mzungu na kuniambia nijifanye ninazo dawa zakuwauzia na nilipopiga kweli alinipokea na kuniambia niende hotelini.

“Kule walinihoji kwa ukali kama kweli nitawaletea dawa halisi, huku akidai kuwa anaogopa sifa mbaya za utapeli kutoka kwa Watanzania,” alisema na kuongeza;

“Yule mzungu alionekana mwenye fedha nyingi, kwani nilikuta ‘briefcase’ ndogo ikiwa imejaa dola, na akanitaka nipige picha yangu, na kisha nimletee kwanza sampuli mbili za dawa zenyewe”.

Anasema hata baada ya kukamilisha, aliwasiliana na yule mtu wa kampuni ya dawa ambaye alimwambia kuwa hawezi kumuuzia dawa kidogo, badala yake kama anataka anunue nusu ya mzigo uliotakiwa ambao ni shs milioni 40.

Mwanamke huyo anasema, wakati akisita, alipigiwa simu na mjerumani huyo, na kumwambia kuwa aachane na sampuli na kama hana uwezo wa kuleta mzigo wote, ajitahidi kuletea nusu kwani ulikuwa unatakiwa haraka siku hiyo hiyo.

“ Martin naye alinihimiza kama kweli bosi wake yule mzungu kaniambia nimpelekee, basi nifanye hivyo haraka na kwamba tutagawana faida nusu kwa nusu.

“Anilinipa hadi namba ya akaunti ya benki, ili nikiishalipwa, nimwekea fedha zake,” alisema.

Hata hivyo, Mariselina anasema, walikubaliana na mtu wa kampuni ya dawa kukutana Mlimani City akiwa na fedha na wakakamilisha ununuzi huo.

“Kwanza nilipoona dawa hizo, nilimpigia Martin na kumsomea maandishi yake na namna zilivyofungwa na akakubali kuwa ndizo zenyewe, hivyo nifanye haraka kununua na kuzipeleka kwa mzungu kabla ya saa tisa alasiri.

“Ajabu, nilipofika katika hoteli ile na kupiga namba ya mzungu kumtaarifu kuwa nimefika, simu ilikuwa imezimwa. Nikampigia Martin, nae yake ilikuwa kimya, na hata nilipopiga kwa yule mtu wa kampuni ya dawa, nayo ilikuwa imezimwa,” anasema.

Mariselina anasema, alijaribu kuuliza wafanyakazi wa hoteli ile, ambao walishindwa kutambua kuwepo kwa mgeni mjerumani mahali hapo.

Mwanamke huyo anasema hisia za kuibiwa ziliingia akilini, na kulazimika kukimbilia polisi.

“Jambo la kushangaza, nilipowaambia pale Central, askari waliyekuwapo walicheka na kuniambia, mama umeibiwa ndio mchezo wa huyo mzungu na kwamba ameshawaibia watu wengi kwa mtindo huo.”

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova hakuweza kupatikana baada ya simu yake kuita muda mwingi bila kupokelewa.

Hata hivyo, ofisa mmoja wa polisi aliyezungumza kwa sharti la kutotajwa jina, alisema mjerumani huyo anasakwa kwa matukio hayo, akishirikiana na Watanzania wengine watatu.

“Amewaliza wengi. Anawatumia watu watatu ambao karibuni tutawatia mikononi,” alisema.
Wengine watumia SMS.

Katika hatua isiyoeleweka, watu wasiojulikana wamekuwa wakiwatumia watu mbalimbali jijini Dar es Salaam, jumbe zenye kuwataka kuwasiliana nao kwa madai ya kufanya biashara nao.

Watu hao ambao wanadai kuwa na makazi maeneo ya Sinza, lakini bila kuonesha wanamiliki kampuni gani mara kadhaa wameingilia namba za watu na kuwaomba kuwasiliana nao na kufika katika eneo hilo ili kufanya biashara ambazo hazitajwi.

Moja ya jumbe zinazotumwa kwa watu zinasema kupitia namba 0653634042 na 0767945946; ‘ Habari, …(wanataja jina lako) kampuni yetu imepata namba yako kuwa unaweza kufanya kazi nasi kwa muda wako wa ziada. Kwa maelezo zaidi, wasiliana kwa namba 0653634042 au 0716334595.

Hata hivyo, mmoja wa watu waliowahi kutumiwa ujumbe huo, Violeth Bago wiki iliyopita akiandamana na watu wengine wawili, kweli alikoelekezwa, lakini katika namna ya kushangaza, watu hao walidai kuwa amechelewa kufika, hivyo afike tena kesho yake saa 5 asubuhi kwa majadiliano.

Hata hivyo, watu hao hawasemi ni kampuni gani na inahusiana na biashara gani, hali inayotia mashaka ya uhalali wao.Chanzo;Tanzania Daima

USHUHUDA

Mmiliki na Mhariri Mkuu wa Blogu hii, Bw. John Badi naye amekutana na sakata hili baada ya kupigiwa simu takribani wiki mbili zilizopita na mtu mmoja aliyejitambulisha kwa jina moja la Dk. Alen akitumia namba ya simu ya kiganjani 0763400434 na kudai yupo katika Hifadhi ya Serengeti.

Maelezo ya Dr. huyu feki hayana tofouti na maelezo yaliyotolewa hapo juu, aliniunganisha na Boss wake alidai kuwa ni Operation Manager naye kunipa maelekezo nikatafute hizo dawa aina ya Gustavic Animal Vaccination 1000mls, 68f made in Germany na kunipa na ya mtu aliyemwita Dk. Alimu Rashid mwenye namba za simu 0783022991 na nitoe order ya pair 50 za hizo dawa.

Cha kushangaza safari hii huyu alitumia namba ya simu 0712210078 siyo ile ya Dr. Alen tena, basi alinielekeza nikisha zipata hizo dawa niende Double Tree Hotel kule Masaki ili nionane na huyo mzungu mjerumani.

Lakini kutokana na upeo wangu wa haraka haraka nilishitukia ile Deal kwani nilijiuliza maswali kadhaa kichwani, inakuwaje mtu tu from no where aje anipe mimi deal la mamilioni? Na hata kama yupo huko Serengeti Je yeye hana ndugu au rafiki wa karibu hapa Dar wa kufanya nae Deal? Hihi kweli Deal la Mamilioni mtu anashindwa kupanda ndege kutoka Serengeti hadi Dar akasimamia Deal then akarudi huko? maswali haya na mengine mengi ndio yaliyoniokoa nisiingie katika mkenge huo.

TAHADHALI
Daily Mitikasi Blog inawatahadhalisha wasomaji wake na wananchi wote kwa ujumla kuwa makini na vishawishi mbalimbali vya utajiri wa haraka haraka... bali waendelee kujibidiisha katika shughuli zao za kila siku iko siku utajiri wataupata kwa jasho lao na si vinginevyo.

6 comments:

Anonymous said...

This Guys their still at work and their numbers are registered but it seems their names are fake names.

They called me today with the same scenario but thanks To God I prayed and my heart was so heavy to do it. Their Changing Numbers everyday.

So my opinion TCRA should review the registration of this card

Unknown said...

Oh my God mimi pia sasa ivi ndio naongea nao ila sjui niende Polis au vp nilipata mashaka ndio nikagoogle

Unknown said...

Oh my God mimi pia sasa ivi ndio naongea nao ila sjui niende Polis au vp nilipata mashaka ndio nikagoogle

Unknown said...

Oh my God mimi pia sasa ivi ndio naongea nao ila sjui niende Polis au vp nilipata mashaka ndio nikagoogle

Unknown said...

Oh my God mimi pia sasa ivi ndio naongea nao ila sjui niende Polis au vp nilipata mashaka ndio nikagoogle

Anonymous said...

Hawa jamaa ni wajinga wamenipigia ikanibid ni google kwanz hiyo dawa na bei yake amenambia ni milion kwa chupa moja