Na Anna Nkinda –
Maelezo, Lindi
Mjumbe wa
Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupitia wilaya ya
Lindi mjini Mama Salma Kikwete (pichani), ameitaka jamii kutumia sauti zao kuwasemea watoto wenye mahitaji maalum kwani
watoto hao wanakabiliwa na changamoto
mbalimbali na hawana mtu wa kumwambia matatizo yao.
Mama Kikwete ambaye ni
Mke wa Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alitoa rai hiyo jana alipotembelea
kitengo cha wanafunzi wenye mahitaji maalum kilichopo shule ya Msingi Mpilipili
wilaya ya Lindi mjini.
Alisema watoto wenye
mahitaji maalum wanakabiliwa na changamoto nyingi ukilinganisha na watoto
wengine pia matatizo yao hayafanani hivyo
basi ni jukumu la kila mtu katika jamii kuwasaidia watoto hao ili waweze kuishi
kama watoto wengine.
“Katika kitengo hiki
kuna watoto wenye tatizo la usonji (Autism) na wasiosikia (viziwi), kila mtoto anahitaji
lake na pale anapokabiliwa na tatizo
anatakiwa kusaidiwa kwa haraka ili
asijisikie kunyanyapaliwa. Nawapongeza walimu mnaowafundisha watoto hawa kwani
kazi hii ni ngumu na inahitaji moyo wa ziada”, alisema Mama Kikwete.
Akisoma taarifa ya
kitengo cha wanafunzi wenye mahitaji maalum mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mpilipili
Fadhili Mtitima alisema kitengo hicho kilianzishwa mwaka 1993 kikiwa na
wanafunzi watano na hivi sasa kuna wanafunzi 20 wenye tatizo la usonji 16 kati
yao wavulana ni 16 na wasichana wawili na wasiosikia (viziwi) wawili msichana mmoja
na mvulana mmoja.
Mwalimu Mtitima alisema
njia zinazotumika kuwapata wanafunzi hao ni wanafunzi wa kawaida kutoa taarifa ya
uwepo wa watoto wenye mahitaji maalum katika mitaa yao kwa walimu, wazazi ambao
wamehamasika huwaleta watoto kujiunga na shule, kutoa hamasa na matangazo kwa
jamii katika maadhimisho ya wiki ya elimu kwa wote na kupitia sensa ya watoto inayofanyika
kila mwaka.
“Changamoto
zinazotukabili ni watoto wengi wanaoishi mbali na kitengo wanakosa fursa ya
kupata elimu kutokana na umbali uliopo, baadhi ya wazazi wa watoto wenye
ulemavu hawawaandikishi watoto wao wakiwa na imani kuwa watoto hawa
hawafundishiki, idadi ya walimu haitoshelezi kwani kuna walimu wawili kati ya wanne
wanaohitajika kufundisha watoto wenye tatizo la usonji.
“Kitengo hakina mwalimu
mtaalamu wa elimu ya walemavu wasiosikia na walimu kutojitokeza kujiendeleza
katika mafunzo ya kufundisha wanafunzi wenye mahitaji maalum”, alisema Mwalimu
Mtitima.
Akiwa shuleni hapo Mama
Kikwete aliwaita na kuwasalimia wanafunzi wa kawaida na kuwahimiza kusoma kwa
bidii, kufuata sheria za shule na kuwatii walimu wao kwa kufanya hivyo
watafanya vizuri katika masomo yao na kufika hadi elimu ya Chuo kikuu.
“Licha ya kusoma kwa
bidii na kuhudhuria darasani mwanafunzi bora anatakiwa kuwahi shuleni na kufanya
kazi za shule ikiwa ni pamoja na kusafisha eneo lake”, alisisitiza.
No comments:
Post a Comment