Tangazo

June 16, 2012

MWENGE WA UHURU WAWASILI ZANZIBAR UKITOKEA MKOANI LINDI

Na Mohammed Mhina, wa Jeshi la Polisi

Mwenge wa Uhuru jana Juni 15, Umeingia Kisiwani Zanzibar ambapo Kiongozi wa Mbio za Mwenge Kitaifa Kapteni Honest Mwanossa ameweka mawe ya msingi na kuzindua miradi mbali mbali ya maendeleo katika mkoa wa mjini Magharibi.

Akiweka jiwe la Msingi la kituo kidogo cha Polisi cha Kombeni Mjini Zanzibar, kiongozi huyo amewataka viongozi wa Kitaifa kuepuka ufujaji wa fedha za wananchi na kujiingiza kwenye ufisadi na kuwataka wafanye mambo kwa maslahi ya Taifa.

Awali katika risala yao kwa Kiongozi wa mbio za Mwenge, wananchi wa Makombeni wameliomba Jeshi la Polisi kuangalia uwezekano wa kuharakisha ujenzi wa kituo hicho ili kupunguza kero ya uhalifu katika eneo hilo.

Moja ya ujumbe wa Mwenge wa mwaka huu umehimiza umuhimu wa kila mmoja wetu kuhesabiwa katika Sensa ya kitaifa ili kuiwezesha Serikali kupanga vema maendeleo kwa wananchi wake. 

Mwenge huo umewasili kisiwani Zanzibar ukiotokea mkoa wa Lindi ambako ulikuwa ukikimbizwa katika wilaya mbalimbali za mkoa huo.

Ukiwa Kisiwani hapa, Kiongozi wa Mbio za Mwenge Kitaifa atazindua na kuweka mawe ya msingi ya miradi mbalimbali ya maendeleo katika wilaya na mikoa yote mitano ya Unguja na Pemba kabla ya kuendelea na mbio zake katika mikoa mingine ya Tanzania Bara.

No comments: