Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Saidi Mecki Sadiki |
Na. Aron Msigwa
–MAELEZO.
Dar es
salaam.
Zikiwa zimebaki siku
chache Tanzania iungane na mataifa mengine kuadhimisha siku ya Wanawake duniani
, Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Mh. Saidi Meck Sadiki ameeleza kuwa ipo haja ya
jamii, Asasi za kiraia na zile za kidini
kushiriki kikanilifu katika kuweka
mikakati ya kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili wanawake
nchini.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani
yatakayofanyika tarehe 8 mwezi huu Mh. Sadiki Meck Sadiki ameeleza kuwa licha ya mchango mkubwa wanaoutoa katika
maendeleo ya taifa wanawake wanakabiliana na changamoto mbalimbali kutoka
katika jamii inayowazunguka.
Amesema licha ya wanawake
kuwa na jukumu la kutunza familia, kuendesha shughuli za uzalishaji wa bidhaa
na huduma mbalimbali kutokana na shughuli za ujasiriamali bado wanakabiliwa na
changamoto za maradhi, vifo vitokanavyo na uzazi, kupigwa, kutukanwa,
kutelekezwa, kubakwa, kuandamwa na vitendo vya ukeketaji na mauaji ya vikongwa.
Amezitaja changamoto
nyingine kuwa ni pamoja na kunyimwa haki ya kumiliki mali, kutoshirikishwa na
kutopewa haki sawa katika ngazi za maamuzi na kuongeza kuwa wakati umefika sasa
kwa jamii kutambua na kuthamini mchango walio nao kijamii, kisiasa na kiuchumi
kwa kuwapa wanawake fursa sawa katika nyanja zote.
“ Siku
ya Wanawake duniani inaongozwa na Kauli mbiu isemayo, Chochea Mabadiliko Kuleta
Usawa Kijinsia , ujumbe huu unaelimisha na kuhamasisha jamii, Serikali, Asasi
za Kiraia na za Kidini kutambua umuhimu wa kushirikiana wanaume na wanawake
katika ngazi zote za maendeleo”
Ameeleza kuwa jiji la
Dar es salaam litaungana na maeneo mengine nchini katika kuiadhimisha siku hiyo
muhimu kwa maadhimisho makubwa yatakayofanyika katika uwanja wa Mwembeyanga katika Halmashauri ya Manispaa ya Temeke huku
mgeni rasmi akiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na
Serikali za Mitaa Hawa Ghasia.
Katika hatua nyingine
Mh. Meki Sadiki amewataka wakazi wa jiji la Dar es salaam hususan wale
wanaoishi katika maeneo hatarishi yanayokumbwa na mafuriko mara kwa mara kutii
taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kwa kuondoka katika maeneo hayo
kufuatia mvua kubwa zinazoendelea kunyesha nchini ili kuepuka madhara
yanayoweza kuepukika.
Akitoa taarifa kuhusu
mikakati ya kukabiliana na majanga yanayoweza kutokea wakati wa msimu wa mvua
kama ilivyotabiriwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Mh. Meck Sadiki ameeleza kuwa
tayari serikali imejipanga chini ya kitengo cha Maafa cha Ofisi ya Waziri Mkuu
kwa kuwa na kikosi kazi kinachohusisha
vikosi vya ulinzi na usalama vya majeshi ya Tanzania.
Ameeleza kuwa serikali
kwa kuthamini umuhimu wa maisha ya raia wake hasa wale waishio mabondeni
imekuwa ikitoa taarifa za kuhama mapema lakini baadhi yao hugoma kuyahama maeno
yao na pindi wanapoondolewa kwa nguvu huamua kwenda mahakamani kuishitaki
serikali.
“Mara nyingi tumekuwa
tukiwataka mara kwa mara wale wote wanaoishi bondeni kuhama sio tu wakati wa
msimu wa mvua lakini wenzetu wamekua wakiona suluhisho lao ni kukimbilia
mahakamani jambo ambalo linasababisha mahakama kusimamisha zoezi letu kama
tunavyojua serikali yetu inaheshimu uhuru wa mahakama”
Kuhusu kesi
zilizopelekwa mahakamani kuhusiana na zoezi la kuwaondoa wananchi wanaoishi
katika bonde la mto Msimbazi amesema tayari kuna kesi nne zinazoendelea kushughulikiwa na tayari
Manispaa ya Ilala imeshinda kesi moja.
Ametoa wito kwa
wananchi kuchukua tahadhari katika kipindi hiki ikiwemo kutoa taarifa za
matukio yanayohatarisha maisha na kujenga tabia ya kushirikiana katika kutatua
changamoto zinazoweza kujitokeza pia
kutoa taarifa kwa mamlaka husika pindi wanapoona baadhi ya watu wanajenga
katika maeneo yasiyoruhusiwa.
No comments:
Post a Comment