Tangazo

October 11, 2013

Wanafunzi wasichana wa VETA watakiwa kuwa ngangari katika masomo

Mama Kikwete
Na Anna Nkinda – Maelezo, Lindi

Wanafunzi wa kike wa Vyuo vya Mafunzo  na Elimu ya Ufundi Stadi (VETA) wametakiwa kutoogopa kusoma masomo magumu yanayosomwa na watoto wa kiume kwani hata wao wanauwezo wa kufanya hivyo na kwa kujifunza kwao fani hizo wataweza kupata ajira kirahisi.

Wito huo umetolewa jana na Mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati wa uzinduzi wa awamu ya pili ya mradi wa VETA  kwa ajili ya sekta ya gesi na mafuta ya petroli wenye madhumuni ya kuimarisha ajira kwa vijana kupitia ufundi stadi uliofanyika katika chuo cha VETA mkoani Lindi

Mama Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) akiwa chuoni hapo alitembelea  karakana ya chuo hicho na kujionea wanafunzi wakijifunza kwa vitendo  ufundi wa magari, umeme, useremala  na masomo ya kompyuta wanafunzi wote katika madarasa hayo ni wa kiume kasoro darasa la ufundi umeme ambako alimkuta mwanafunzi wa kike mmoja.

Pia katika darasa la kompyuta kulikuwa na idadi kubwa ya wanafunzi wa kike hii inaonyesha kuwa wanafunzi wengi wa kike wanapenda kusoma masomo ya ukatibu mahsusi  (muhtasi)  ambayo wanaona kuwa ni rahisi kwao na kuyakimbia yale ambayo ni magumu kwa kudhani kuwa hawawezi kusoma.

“Chuo cha VETA Lindi kina jumla ya wanafunzi 224 kati ya hao wasichana ni 63, kutokana na upatikanaji wa rasilimali zilizopo katika mikoa ya Kusini Shirika la Madini limefadhili wanachuo 64 kati ya hao wasichana ni 11 mimi kama mzazi na mdau wa maendeleo wa mkoa huu nauliza tuko wapi na je tutafika?, alihoji Mama Kikwete.

Mwenyekiti huyo wa WAMA alisema makusudio ya VETA ni kuona kijana akimaliza mafunzo yake anaweza kujiajiri lengo likiwa ni kuwaondoa vijana wengi kutoka kwenye eneo lisilo la ajira na kupata ajira kwani  si lazima mtu aajiriwe ofisini na kuwataka wasome kwa bidii ili waweze kufika mbali.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa huo Ludovick Mwananzila alisema ugunduzi wa gesi katika mikoa ya Kusini ni kitu kipya nchini hivyo basi wananchi bila ya kupewa mafunzo fani hiyo inaweza kutoweka.

Alisema chuo hicho kama kitatumika vizuri kitakuwa ni mkombozi mkubwa kwa wananchi wa mkoa huo na kuwaomba wazazi kuwa tayari kuwapeleka watoto wao choni hapo kwani wataweza kuajiriwa au kujiajiri wenyewe pindi watakapomaliza mafunzo yao na hivyo kujikwamua na hali ngumu ya maisha.

Mkurugenzi Mkuu wa VETA nchini Mhandisi Zebadiah Moshi alizishukuru kampuni za British Gas ya Uingereza ambao wametoa mchango wa kuimarisha  mafunzo kwa wanafunzi katika vyuo vya Lindi na Mtwara na Voluntary Services Organisation (VSO Tanzania) ambao ndiyo wanaratibu mafunzo hayo.

Mhandisi huyo alisema chuo hicho ndicho kinachonufaika zaidi na mafunzo hayo  kwani yataboresha mafunzo ya elimu kutokana na ushirikiano uliopo, walimu watajengewa uwezo katika mafunzo na wanafunzi watakaomaliza katika vyuo hivyo watakuwa na umahiri mkubwa zaidi.

Alisema,“Vyuo vyetu vitapata vifaa vya kisasa vya kufundishia na mafunzo haya yatakuwa ya kiwango kizuri. Tunaahidi kuimarisha uhusiano uliopo na tutasimamia na kuhakikisha kuwa uhusiano huu unatimiza  malengo yaliyokusudiwa”.

Kwa upande wao baadhi ya wanafunzi wa chuo hicho kutoka Mtwara na Lindi ambao walitoa ushuhuda  jinsi walivyoweza kunufaika na mafunzo ya VETA walisema watu wengi wanaposikia kijana anaenda kusoma hapo wanamdharau na kuona  kuwa ameshindwa kila kitu katika maisha na kukimbilia huko jambo ambalo si kweli kwani  mafunzo wanayopewa ni mazuri na yanawasaidia katika maisha yao.

“Tunaiomba Serikali iongeze idadi ya wanafunzi wanaojiunga na vyuo hivi hii itawasaidia vijana wenzetu ambao tunakutana nao mitaani kipindi cha likizo, vijana hawa ni wengi na hawana ajira ili nao waweze kupata elimu kama hii tunayoipata sisi kwani pindi wakimaliza mafunzo yao wataweza kujiajiri au kuajiriwa”, walisema wanafunzi hao.

Mradi huo ambao ni wa miaka miwili kuanzia mwaka 2013 hadi 2015 umeanzishwa na kuendelezwa na kampuni ya British Gas ya Uingereza, Voluntary Services Organisation (VSO Tanzania) , wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Serikali ya Uingereza kupitia idara yake ya Maendeleo ya Kimataifa(DFID) British Council na VETA utatoa mafunzo kwa zaidi ya wanafunzi 224 kutoka kwa walimu wenye uzoefu wa kimataifa kwa kushirikiana na walimu wao na kukifanya chuo hicho kufikia viwango vya kimataifa.

Pia utaboresha matumizi ya lugha ya kiingereza kwa walimu 15 kwa sababu vijana watakaowafundisha wanatarajiwa kuajiriwa katika makampuni ya ndani na ya kimataifa, hivyo lugha ya kiingereza ni nyenzo muhimu ya mawasiliano na walimu wanne kutoka karakana nne za chuo hicho  watajengwa uwezo kwa kupewa kozi zenye hadhi ya kimataifa ili wapate tuzo zinazotambulika kitaifa.

Awamu ya kwanza ya mradi huo ulizinduliwa mwishoni mwa mwaka 2012 katika chuo cha Ufundi VETA Mtwara na Makamu wa Rais Dk. Gharib Bilal.

No comments: